0:00
0:00

Mlango 97

Bwana ametamalaki, nchi na ishangilie, Visiwa vingi na vifurahi.
2 Mawingu na giza vyamzunguka, Haki na hukumu ndio msingi wa kiti chake.
3 Moto hutangulia mbele zake, Nao huwateketeza watesi wake pande zote.
4 Umeme wake uliuangaza ulimwengu, Nchi ikaona ikatetemeka.
5 Milima iliyeyuka kama nta mbele za Bwana, Mbele za Bwana wa dunia yote.
6 Mbingu zimetangaza haki yake, Na watu wote wameuona utukufu wake.
7 Na waaibishwe wote waabuduo sanamu, Wajivunao kwa vitu visivyofaa; Enyi miungu yote, msujuduni Yeye.
8 Sayuni imesikia na kufurahi, Binti za Yuda walishangilia, Kwa sababu ya hukumu zako, Ee Bwana.
9 Maana Wewe, Bwana, ndiwe Uliye juu, Juu sana kuliko nchi yote; Umetukuka sana juu ya miungu yote.
10 Enyi mmpendao Bwana, uchukieni uovu; Huwalinda nafsi zao watauwa wake, Na kuwaokoa na mkono wa wasio haki.
11 Nuru imemzukia mwenye haki, Na furaha wanyofu wa moyo.
12 Enyi wenye haki, mmfurahieni Bwana, Na kulishukuru jina lake takatifu.