0:00
0:00

Mlango 145

Ee Mungu wangu, Mfalme, nitakutukuza, Nitalihimidi jina lako milele na milele.
2 Kila siku nitakuhimidi, Nitalisifu jina lako milele na milele.
3 Bwana ndiye mkuu mwenye kusifiwa sana, Wala ukuu wake hautambulikani.
4 Kizazi kwa kizazi kitayasifu matendo yako, Kitayatangaza matendo yako makuu.
5 Nitaifikiri fahari ya utukufu wa adhama yako, Na matendo yako yote ya ajabu.
6 Watu watayataja matendo yako ya kutisha, Nami nitausimulia ukuu wako.
7 Watalihubiri kumbukumbu la wema wako mkuu. Wataiimba haki yako.
8 Bwana ana fadhili, ni mwingi wa huruma, Si mwepesi wa hasira, ni mwingi wa rehema,
9 Bwana ni mwema kwa watu wote, Na rehema zake zi juu ya kazi zake zote.
10 Ee Bwana, kazi zako zote zitakushukuru, Na wacha Mungu wako watakuhimidi.
11 Wataunena utukufu wa ufalme wako, Na kuuhadithia uweza wako.
12 Ili kuwajulisha watu matendo yake makuu, Na utukufu wa fahari ya ufalme wake.
13 Ufalme wako ni ufalme wa zamani zote, Na mamlaka yako ni ya vizazi vyote.
14 Bwana huwategemeza wote waangukao, Huwainua wote walioinama chini.
15 Macho ya watu wote yakuelekea Wewe, Nawe huwapa chakula chao wakati wake.
16 Waufumbua mkono wako, Wakishibisha kila kilicho hai matakwa yake.
17 Bwana ni mwenye haki katika njia zake zote, Na mwenye fadhili juu ya kazi zake zote.
18 Bwana yu karibu na wote wamwitao, Wote wamwitao kwa uaminifu.
19 Atawafanyia wamchao matakwa yao, Naye atakisikia kilio chao na kuwaokoa.
20 Bwana huwahifadhi wote wampendao, Na wote wasio haki atawaangamiza.
21 Kinywa changu kitazinena sifa za Bwana; Wote wenye mwili na walihimidi jina lake takatifu milele na milele.