0:00
0:00

Mlango 76

Katika Yuda Mungu amejulikana, Katika Israeli jina lake ni kuu.
2 Kibanda chake pia kiko Salemu, Na maskani yake iko Sayuni.
3 Huko ndiko alikoivunja mishale ya uta, Ngao, na upanga, na zana za vita.
4 Wewe U mwenye fahari na adhama, Toka milima ya mateka.
5 Wametekwa wenye moyo thabiti; Wamelala usingizi; Wala hawakuiona mikono yao Watu wote walio hodari.
6 Kwa kukemea kwako, Ee Mungu wa Yakobo, Gari na farasi wameshikwa na usingizi mzito.
7 Wewe ndiwe utishaye, naam, Wewe; Naye ni nani awezaye kusimama ufanyapo hasira?
8 Toka mbinguni ulitangaza hukumu; Nchi iliogopa, ikakaa kimya.
9 Mungu aliposimama ili kuhukumu Na kuwaokoa wapole wa dunia wote pia.
10 Maana hasira ya binadamu itakusifu, Masalio ya hasira utajifunga kama mshipi.
11 Wekeni nadhiri, mkaziondoe Kwa Bwana, Mungu wenu. Wote wanaomzunguka wamletee hedaya, Yeye astahiliye kuogopwa.
12 Yeye huzikata roho za wakuu; Na kuwatisha wafalme wa dunia.