0:00
0:00

Mlango 132

Bwana, umkumbukie Daudi Taabu zake zote alizotaabika.
2 Ndiye aliyemwapia Bwana, Akaweka nadhiri kwa Shujaa wa Yakobo.
3 Sitaingia hemani mwa nyumba yangu, Wala sitapanda matandiko ya kitanda changu;
4 Sitaacha macho yangu kuwa na usingizi, Wala kope zangu kusinzia;
5 Hata nitakapompatia Bwana mahali, Na Shujaa wa Yakobo maskani.
6 Tazama, tulisikia habari zake katika Efrata, Katika konde la Yearimu tuliiona.
7 Na tuingie katika maskani yake, Tusujudu penye kiti cha kuwekea miguu yake.
8 Ee Bwana, uinuke, uende kwenye raha yako, Wewe na sanduku la nguvu zako.
9 Makuhani wako na wavikwe haki, Watauwa wako na washangilie.
10 Kwa ajili ya Daudi, mtumishi wako, Usiurudishe nyuma uso wa masihi
11 Bwana amemwapia Daudi neno la kweli, Hatarudi nyuma akalihalifu, Baadhi ya wazao wa mwili wako Nitawaweka katika kiti chako cha enzi.
12 Wanao wakiyashika maagano yangu, Na shuhuda nitakazowafundisha; Watoto wao nao wataketi Katika kiti chako cha enzi milele.
13 Kwa kuwa Bwana ameichagua Sayuni, Ameitamani akae ndani yake.
14 Hapo ndipo mahali pangu pa raha milele, Hapo nitakaa kwa maana nimepatamani.
15 Hakika nitavibariki vyakula vyake Wahitaji wake nitawashibisha chakula.
16 Na makuhani wake nitawavika wokovu, Na watauwa wake watashangilia.
17 Hapo nitamchipushia Daudi pembe, Na taa nimemtengenezea masihi wangu.
18 Adui zake nitawavika aibu, Bali juu yake taji yake itasitawi.