0:00
0:00

Mlango 148

Haleluya. Msifuni Bwana kutoka mbinguni; Msifuni katika mahali palipo juu.
2 Msifuni, enyi malaika wake wote; Msifuni, majeshi yake yote.
3 Msifuni, jua na mwezi; Msifuni, nyota zote zenye mwanga.
4 Msifuni, enyi mbingu za mbingu, Nanyi maji mlioko juu ya mbingu.
5 Na vilisifu jina la Bwana, Kwa maana aliamuru, vikaumbwa.
6 Amevithibitisha hata milele na milele, Ametoa amri wala haitapita.
7 Msifuni Bwana kutoka nchi, Enyi nyangumi na vilindi vyote.
8 Moto na mvua ya mawe, theluji na mvuke, Upepo wa dhoruba ulitendao neno lake.
9 Milima na vilima vyote, Miti yenye matunda na mierezi yote.
10 Hayawani, na wanyama wafugwao, Vitambaavyo, na ndege wenye mbawa.
11 Wafalme wa dunia, na watu wote, Wakuu, na makadhi wote wa dunia.
12 Vijana waume, na wanawali, Wazee, na watoto;
13 Na walisifu jina la Bwana, Maana jina lake peke yake limetukuka; Adhama yake i juu ya nchi na mbingu.
14 Naye amewainulia watu wake pembe, Sifa za watauwa wake wote; Wana wa Israeli, watu walio karibu naye. Haleluya.