0:00
0:00

Mlango 26

Ee Bwana, unihukumu mimi, Maana nimekwenda kwa ukamilifu wangu, Nami nimemtumaini Bwana bila wasiwasi.
2 Ee Bwana, unijaribu na kunipima; Unisafishe mtima wangu na moyo wangu.
3 Maana fadhili zako zi mbele ya macho yangu, Nami nimekwenda katika kweli yako.
4 Sikuketi pamoja na watu wa ubatili, Wala sitaingia mnamo wanafiki.
5 Nimelichukia kusanyiko la watenda mabaya, Wala sitaketi pamoja na watu waovu.
6 Nitanawa mikono yangu kwa kutokuwa na hatia, Na kuizunguka madhabahu yako, Ee Bwana
7 Ili niitangaze sauti ya kushukuru, Na kuzisimulia kazi zako za ajabu.
8 Bwana, nimependa makao ya nyumba yako, Na mahali pa maskani ya utukufu wako.
9 Usiiondoe nafsi yangu pamoja na wakosaji, Wala uhai wangu pamoja na watu wa damu.
10 Mikononi mwao mna madhara, Na mkono wao wa kuume umejaa rushwa.
11 Ila mimi nitakwenda kwa ukamilifu wangu; Unikomboe, unifanyie fadhili.
12 Mguu wangu umesimama palipo sawa; Katika makusanyiko nitamhimidi Bwana.