0:00
0:00

Mlango 5

Ee Bwana, uyasikilize maneno yangu, Ukuangalie kutafakari kwangu.
2 Uisikie sauti ya kilio changu, Ee Mfalme wangu na Mungu wangu, Kwa maana Wewe ndiwe nikuombaye.
3 Bwana, asubuhi utaisikia sauti yangu, Asubuhi nitakupangia dua yangu na kutazamia.
4 Maana huwi Mungu apendezwaye na ubaya; Mtu mwovu hatakaa kwako;
5 Wajivunao hawatasimama mbele za macho yako; Unawachukia wote watendao ubatili.
6 Utawaharibu wasemao uongo; Bwana humzira mwuaji na mwenye hila
7 Bali mimi, kwa wingi wa fadhili zako, Nitaingia nyumbani mwako; Na kusujudu kwa kicho, Nikilielekea hekalu lako takatifu.
8 Bwana, uniongoze kwa haki yako, Kwa sababu yao wanaoniotea. Uisawazishe njia yako mbele ya uso wangu,
9 Maana vinywani mwao hamna uaminifu; Mtima wao ni shimo tupu, koo lao ni kaburi wazi, Ulimi wao hujipendekeza.
10 Wewe, Mungu, uwapatilize, Na waanguke kwa mashauri yao. Uwatoe nje kwa ajili ya wingi wa makosa yao, Kwa maana wamekuasi Wewe.
11 Nao wote wanaokukimbilia watafurahi; Watapiga daima kelele za furaha. Kwa kuwa Wewe unawahifadhi, Walipendao jina lako watakufurahia.
12 Kwa maana Wewe utambariki mwenye haki; Bwana, utamzungushia radhi kama ngao.