0:00
0:00

Mlango 16

Mungu, unihifadhi mimi, Kwa maana nakukimbilia Wewe.
2 Nimemwambia Bwana, Ndiwe Bwana wangu; Sina wema ila utokao kwako.
3 Watakatifu waliopo duniani ndio Walio bora, Hao ndio niliopendezwa nao.
4 Huzuni zao zitaongezeka Wambadilio Mungu kwa mwingine; Sitazimimina sadaka zao za damu, Wala kuyataja majina yao midomoni mwangu.
5 Bwana ndiye fungu la posho langu, Na la kikombe changu; Wewe unaishika kura yangu.
6 Kamba zangu zimeniangukia mahali pema, Naam, nimepata urithi mzuri.
7 Nitamhimidi Bwana aliyenipa shauri, Naam, mtima wangu umenifundisha usiku.
8 Nimemweka Bwana mbele yangu daima, Kwa kuwa yuko kuumeni kwangu, sitaondoshwa.
9 Kwa hiyo moyo wangu unafurahi, Nao utukufu wangu unashangilia, Naam, mwili wangu nao utakaa kwa kutumaini.
10 Maana hutakuachia kuzimu nafsi yangu, Wala hutamtoa mtakatifu wako aone uharibifu.
11 Utanijulisha njia ya uzima; Mbele za uso wako ziko furaha tele; Na katika mkono wako wa kuume Mna mema ya milele.