0:00
0:00

Mlango 37

Usikasirike kwa sababu ya watenda mabaya, Usiwahusudu wafanyao ubatili.
2 Maana kama majani watakatika mara, Kama miche mibichi watanyauka.
3 Umtumaini Bwana ukatende mema, Ukae katika nchi, upendezwe na uaminifu.
4 Nawe utajifurahisha kwa Bwana, Naye atakupa haja za moyo wako.
5 Umkabidhi Bwana njia yako, Pia umtumaini, naye atafanya.
6 Ataitokeza haki yako kama nuru, Na hukumu yako kama adhuhuri.
7 Ukae kimya mbele za Bwana, Nawe umngojee kwa saburi; Usimkasirikie yeye afanikiwaye katika njia yake, Wala mtu afanyaye hila.
8 Ukomeshe hasira, uache ghadhabu, Usikasirike, mwisho wake ni kutenda mabaya.
9 Maana watenda mabaya wataharibiwa, Bali wamngojao Bwana ndio watakaoirithi nchi.
10 Maana bado kitambo kidogo asiye haki hatakuwapo, Utapaangalia mahali pake wala hatakuwapo.
11 Bali wenye upole watairithi nchi, Watajifurahisha kwa wingi wa amani.
12 Asiye haki hunuia mabaya juu ya mwenye haki, Na kumsagia meno yake.
13 Bwana atamcheka, Maana ameona kwamba siku yake inakuja.
14 Wasio haki wamefuta upanga na kupinda uta, Wamwangushe chini maskini na mhitaji, Na kuwaua wenye mwenendo wa unyofu.
15 Upanga wao utaingia mioyoni mwao wenyewe, Na nyuta zao zitavunjika.
16 Kidogo alicho nacho mwenye haki ni bora Kuliko wingi wa mali wa wasio haki wengi.
17 Maana mikono ya wasio haki itavunjika, Bali Bwana huwategemeza wenye haki.
18 Bwana anazijua siku za wakamilifu, Na urithi wao utakuwa wa milele.
19 Hawataaibika wakati wa ubaya, Na siku za njaa watashiba.
20 Bali wasio haki watapotea, Nao wamchukiao Bwana watatoweka, Kama uzuri wa mashamba, Kama moshi watatoweka.
21 Asiye haki hukopa wala halipi, Bali mwenye haki hufadhili, hukirimu.
22 Maana waliobarikiwa na yeye watairithi nchi, Nao waliolaaniwa na yeye wataharibiwa.
23 Hatua za mtu zaimarishwa na Bwana, Naye aipenda njia yake.
24 Ajapojikwaa hataanguka chini, Bwana humshika mkono na kumtegemeza.
25 Nalikuwa kijana nami sasa ni mzee, Lakini sijamwona mwenye haki ameachwa Wala mzao wake akiomba chakula.
26 Mchana kutwa hufadhili na kukopesha, Na mzao wake hubarikiwa.
27 Jiepue na uovu, utende mema, Na kukaa hata milele.
28 Kwa kuwa Bwana hupenda haki, Wala hawaachi watauwa wake. Wao hulindwa milele, Bali mzao wa wasio haki ataharibiwa.
29 Wenye haki watairithi nchi, Nao watakaa humo milele.
30 Kinywa chake mwenye haki hunena hekima, Na ulimi wake husema hukumu.
31 Sheria ya Mungu wake imo moyoni mwake. Hatua zake hazitelezi.
32 Mtu asiye haki humvizia mwenye haki, Na kutafuta jinsi ya kumfisha.
33 Bwana hatamwacha mkononi mwake, Wala hatamlaumu atakapohukumiwa.
34 Wewe umngoje Bwana, Uishike njia yake, Naye atakutukuza uirithi nchi, Wasio haki watakapoharibiwa utawaona.
35 Nimemwona mtu asiye haki mkali sana, Akijieneza kama mwerezi wa Lebanoni.
36 Nikapita na kumbe! Hayuko, Nikamtafuta wala hakuonekana.
37 Umwangalie sana mtu mkamilifu, Umtazame mtu mnyofu, Maana mwisho wake mtu huyo ni amani.
38 Wakosaji wataangamizwa pamoja, Wasio haki mwisho wao wataharibiwa.
39 Na wokovu wa wenye haki una Bwana; Yeye ni ngome yao wakati wa taabu.
40 Naye Bwana huwasaidia na kuwaopoa; Huwaopoa na wasio haki na kuwaokoa; Kwa kuwa wamemtumaini Yeye.