0:00
0:00

Mlango 34

Nitamhimidi Bwana kila wakati, Sifa zake zi kinywani mwangu daima.
2 Katika Bwana nafsi yangu itajisifu, Wanyenyekevu wasikie wakafurahi.
3 Mtukuzeni Bwana pamoja nami, Na tuliadhimishe jina lake pamoja.
4 Nalimtafuta Bwana akanijibu, Akaniponya na hofu zangu zote.
5 Wakamwelekea macho wakatiwa nuru, Wala nyuso zao hazitaona haya.
6 Maskini huyu aliita, Bwana akasikia, Akamwokoa na taabu zake zote.
7 Malaika wa Bwana hufanya kituo, Akiwazungukia wamchao na kuwaokoa.
8 Onjeni mwone ya kuwa Bwana yu mwema; Heri mtu yule anayemtumaini.
9 Mcheni Bwana, enyi watakatifu wake, Yaani, wamchao hawahitaji kitu.
10 Wana-simba hutindikiwa, huona njaa; Bali wamtafutao Bwana hawatahitaji kitu cho chote kilicho chema.
11 Njoni, enyi wana, mnisikilize, Nami nitawafundisha kumcha Bwana.
12 Ni nani mtu yule apendezwaye na uzima, Apendaye siku nyingi apate kuona mema?
13 Uuzuie ulimi wako na mabaya, Na midomo yako na kusema hila.
14 Uache mabaya ukatende mema, Utafute amani ukaifuatie.
15 Macho ya Bwana huwaelekea wenye haki, Na masikio yake hukielekea kilio chao.
16 Uso wa Bwana ni juu ya watenda mabaya, Aliondoe kumbukumbu lao duniani.
17 Walilia, naye Bwana akasikia, Akawaponya na taabu zao zote.
18 Bwana yu karibu nao waliovunjika moyo, Na waliopondeka roho huwaokoa.
19 Mateso ya mwenye haki ni mengi, Lakini Bwana humponya nayo yote.
20 Huihifadhi mifupa yake yote, Haukuvunjika hata mmoja.
21 Uovu utamwua asiye haki, Nao wamchukiao mwenye haki watahukumiwa.
22 Bwana huzikomboa nafsi za watumishi wake, Wala hawatahukumiwa wote wamkimbiliao.