0:00
0:00

Mlango 71

Nimekukimbilia Wewe, Bwana, Nisiaibike milele.
2 Kwa haki yako uniponye, uniopoe, Unitegee sikio lako, uniokoe.
3 Uwe kwangu mwamba wa makazi yangu, Nitakakokwenda sikuzote. Umeamuru niokolewe, Ndiwe genge langu na ngome yangu.
4 Ee Mungu wangu, uniopoe mkononi mwa mkorofi, Katika mkono wake mwovu, mdhalimu,
5 Maana ndiwe taraja langu, Ee Bwana MUNGU, Tumaini langu tokea ujana wangu.
6 Nimekutegemea Wewe tangu kuzaliwa, Ndiwe uliyenitoa tumboni mwa mama yangu, Ninakusifu Wewe daima.
7 Nimekuwa kitu cha ajabu kwa watu wengi, Na Wewe ndiwe kimbilio langu la nguvu.
8 Kinywa changu kitajazwa sifa zako, Na heshima yako mchana kutwa.
9 Usinitupe wakati wa uzee, Nguvu zangu zipungukapo usiniache.
10 Kwa maana adui zangu wananiamba, Nao wanaoniotea roho yangu hushauriana.
11 Wakisema, Mungu amemwacha, Mfuatieni, mkamateni, hakuna wa kumponya.
12 Ee Mungu, usiwe mbali nami; Ee Mungu wangu, fanya haraka kunisaidia.
13 Waaibishwe, watoweshwe, adui za nafsi yangu. Wavikwe laumu na aibu wanaonitakia mabaya.
14 Nami nitatumaini daima, Nitazidi kuongeza sifa zake zote.
15 Kinywa changu kitasimulia haki na wokovu wako Mchana kutwa; maana sijui hesabu yake.
16 Nitakuja na mambo ya ajabu ya Bwana MUNGU; Nitawakumbusha watu haki yako Wewe peke yako.
17 Ee Mungu, umenifundisha tokea ujana wangu; Nimekuwa nikitangaza miujiza yako hata leo.
18 Na hata nikiwa ni mzee mwenye mvi, Ee Mungu, usiniache. Hata niwaeleze watu wa kizazi hiki nguvu zako, Na kila atakayekuja uweza wako.
19 Na haki yako, Ee Mungu, Imefika juu sana. Wewe uliyefanya mambo makuu; Ee Mungu, ni nani aliye kama Wewe?
20 Wewe, uliyetuonyesha mateso mengi, mabaya, Utatuhuisha tena. Utatupandisha juu tena Tokea pande za chini ya nchi.
21 Laiti ungeniongezea ukuu! Urejee tena na kunifariji moyo.
22 Nami nitakushukuru kwa kinanda, Na kweli yako, Ee Mungu wangu. Nitakuimbia Wewe kwa kinubi, Ee Mtakatifu wa Israeli.
23 Midomo yangu itafurahi sana nikuimbiapo, Na nafsi yangu uliyoikomboa.
24 Ulimi wangu nao utasimulia Haki yako mchana kutwa. Kwa maana wameaibishwa, Wametahayarika, wanaonitakia mabaya.