0:00
0:00

Mlango 31

Nimekukimbilia Wewe, Bwana, Nisiaibike milele. Kwa haki yako uniponye,
2 Unitegee sikio lako, uniokoe hima. Uwe kwangu mwamba wa nguvu, Nyumba yenye maboma ya kuniokoa.
3 Ndiwe genge langu na ngome yangu; Kwa ajili ya jina lako uniongoze, unichunge.
4 Utanitoa katika wavu walionitegea kwa siri, Maana Wewe ndiwe ngome yangu.
5 Mikononi mwako naiweka roho yangu; Umenikomboa, Ee Bwana, Mungu wa kweli.
6 Nawachukia wao washikao yasiyofaa yenye uongo; Bali mimi namtumaini Bwana.
7 Na nishangilie, nizifurahie fadhili zako, Kwa kuwa umeyaona mateso yangu. Umeijua nafsi yangu taabuni,
8 Wala hukunitia mikononi mwa adui; Miguu yangu umeisimamisha panapo nafasi.
9 Ee Bwana, unifadhili, maana ni katika dhiki, Jicho langu limenyauka kwa masumbufu, Naam, mwili wangu na nafsi yangu.
10 Maana maisha yangu yamekoma kwa huzuni, Na miaka yangu kwa kuugua. Nguvu zangu zinatetemeka kwa uovu wangu, Na mifupa yangu imekauka.
11 Kwa sababu ya watesi wangu nimekuwa laumu, Naam, hasa kwa jirani zangu; Na kitu cha kutisha kwa rafiki zangu; Walioniona njiani walinikimbia.
12 Nimesahauliwa kama mfu asiyekumbukwa; Nimekuwa kama chombo kilichovunjika.
13 Maana nimesikia masingizio ya wengi; Hofu ziko pande zote. Waliposhauriana juu yangu, Walifanya hila wauondoe uhai wangu.
14 Lakini mimi nakutumaini Wewe, Bwana, Nimesema, Wewe ndiwe Mungu wangu.
15 Nyakati zangu zimo mikononi mwako; Uniponye na adui zangu, nao wanaonifuatia.
16 Umwangaze mtumishi wako Kwa nuru ya uso wako; Uniokoe kwa ajili ya fadhili zako.
17 Ee Bwana, nisiaibishwe, maana nimekuita; Waaibishwe wasio haki, wanyamaze kuzimuni.
18 Midomo ya uongo iwe na ububu, Imneneayo mwenye haki maneno ya kiburi, Kwa majivuno na dharau.
19 Jinsi zilivyo nyingi fadhili zako Ulizowawekea wakuchao; Ulizowatendea wakukimbiliao Mbele ya wanadamu!
20 Utawasitiri na fitina za watu Katika sitara ya kuwapo kwako; Utawaficha katika hema Na mashindano ya ndimi.
21 Bwana ahimidiwe; kwa maana amenitendea Fadhili za ajabu katika mji wenye boma.
22 Nami nalisema kwa haraka yangu, Nimekatiliwa mbali na macho yako; Lakini ulisikia sauti ya dua yangu Wakati nilipokulilia.
23 Mpendeni Bwana, Ninyi nyote mlio watauwa wake. Bwana huwahifadhi waaminifu, Humlipa atendaye kiburi malipo tele.
24 Iweni hodari, mpige moyo konde, Ninyi nyote mnaomngoja Bwana.