0:00
0:00

Mlango 48

Basi, haya ndiyo majina ya kabila hizo; toka mwisho wa pande za kaskazini, karibu na njia ya Hethloni, hata maingilio ya Hamathi, hata Hasar-enoni, penye mpaka wa Dameski, yaani, upande wa kaskazini karibu na Hamathi, watakuwa na upande wa mashariki, na upande wa magharibi; Dani fungu moja.
2 Tena mpakani mwake Dani, toka upande wa mashariki hata upande wa magharibi; Asheri, fungu moja.
3 Na mpakani mwa Asheri, toka upande wa mashariki hata upande wa magharibi; Naftali, fungu moja.
4 Na mpakani mwa Naftali, toka upande wa mashariki hata upande wa magharibi; Manase, fungu moja.
5 Na mpakani mwa Manase, toka upande wa mashariki hata upande wa magharibi; Efraimu, fungu moja.
6 Na mpakani mwa Efraimu, toka upande wa mashariki hata upande wa magharibi; Reubeni, fungu moja.
7 Na mpakani mwa Reubeni, toka upande wa mashariki hata upande wa magharibi; Yuda, fungu moja.
8 Na mpakani mwa Yuda, toka upande wa mashariki hata upande wa magharibi, yatakuwapo matoleo mtakayotoa, upana wake mianzi ishirini na tano elfu, na urefu wake sawasawa na moja la mafungu hayo, toka upande wa mashariki hata upande wa magharibi; na mahali patakatifu ni katikati yake.
9 Matoleo hayo, mtakayomtolea Bwana, urefu wake ni mianzi ishirini na tano elfu, na upana wake elfu kumi.
10 Matoleo hayo matakatifu yatakuwa kwa watu hawa, kwa makuhani; upande wa kaskazini urefu wake ishirini na tano elfu, na upande wa magharibi upana wake elfu kumi, na upande wa mashariki upana wake elfu kumi, na upande wa kusini urefu wake ishirini na tano elfu; na mahali patakatifu pa Bwana patakuwa katikati yake.
11 Patakuwa kwa makuhani wa wana wa Sadoki, waliotakasika, walioulinda ulinzi wangu, wasioasi, wana wa Israeli walipoasi, kama Walawi walivyoasi.
12 Na matoleo hayo ya nchi yatolewayo, yatakuwa kwao kitu kitakatifu sana, karibu na mpaka wa Walawi.
13 Na kuukabili mpaka wa makuhani, Walawi watakuwa na fungu, urefu wake ishirini na tano elfu, na upana wake elfu kumi; urefu wote utakuwa ishirini na tano elfu, na upana wake elfu kumi.
14 Wala hawatauza sehemu yake, wala kuibadili, wala hawatawapa wengine malimbuko ya nchi; maana ni matakatifu kwa Bwana.
15 Na mianzi elfu tano iliyosalia katika upana, kuikabili hiyo ishirini na tano elfu, itatumiwa na watu wote, kwa huo mji, na kwa maskani, na kwa viunga, na huo mji utakuwa katikati yake.
16 Na vipimo vyake ni hivi; upande wa kaskazini elfu nne na mia tano, na upande wa kusini elfu nne na mia tano, na upande wa mashariki elfu nne na mia tano, na upande wa magharibi elfu nne na mia tano.
17 Nao mji utakuwa na malisho; upande wa kaskazini mia mbili na hamsini, na upande wa kusini mia mbili na hamsini, na upande wa mashariki mia mbili na hamsini, na upande wa magharibi mia mbili na hamsini.
18 Na mabaki ya urefu wake yaelekeayo matoleo matakatifu, upande wa mashariki yatakuwa elfu kumi, na upande wa magharibi elfu kumi; nayo yatakuwa sawasawa na matoleo matakatifu; na mazao yake yatakuwa ni chakula cha watu wafanyao kazi humo mjini.
19 Na hao wafanyao kazi mjini, wa kabila zote za Israeli, watailima nchi hiyo.
20 Matoleo yote yatakuwa ishirini na tano elfu, kwa ishirini na tano elfu; mtatoa matoleo matakatifu, nchi ya mraba, pamoja na milki ya mji.
21 Nayo mabaki yake yatakuwa ya huyo mkuu, upande huu na upande huu wa matoleo matakatifu, na milki ya mji, kuikabili hiyo ishirini na tano elfu ya matoleo, kuelekea mpaka wa mashariki; tena upande wa magharibi kuikabili hiyo ishirini na tano elfu, upande wa kuelekea mpaka wa magharibi; sawa na yale mafungu, hayo yatakuwa ya huyo mkuu; na matoleo matakatifu na mahali patakatifu pa nyumba patakuwa katikati yake.
22 Tena tokea milki ya Walawi, na tokea milki ya mji, kwa kuwa ni katikati ya nchi iliyo ya mkuu, katikati ya mpaka wa Yuda na mpaka wa Benyamini, itakuwa ya mkuu.
23 Na katika habari za kabila zilizosalia; toka upande wa mashariki hata upande wa magharibi; Benyamini, fungu moja.
24 Tena mpakani mwa Benyamini, toka upande wa mashariki hata upande wa magharibi; Simeoni, fungu moja.
25 Tena mpakani mwa Simeoni, toka upande wa mashariki hata upande wa magharibi; Isakari, fungu moja.
26 Na mpakani mwa Isakari, toka upande wa mashariki hata upande wa magharibi; Zabuloni, fungu moja.
27 Na mpakani mwa Zabuloni, toka upande wa mashariki hata upande wa magharibi; Gadi, fungu moja.
28 Na mpakani mwa Gadi, upande wa kusini kuelekea kusini, mpaka wake utakuwa toka Tamari, mpaka maji ya Meriba-Kadeshi, mpaka kijito cha Misri, mpaka bahari kubwa.
29 Hiyo ndiyo nchi mtakayozigawanyia kabila za Israeli, kuwa urithi wao, na hayo ndiyo mafungu yao, asema Bwana MUNGU.
30 Na matokeo ya mji ndiyo haya; upande wa kaskazini, mianzi elfu nne na mia tano, kwa kupima;
31 na malango ya mji yatatajwa kwa majina ya kabila za Israeli, malango matatu upande wa kaskazini; lango la Reubeni, moja; lango la Yuda, moja; na lango la Lawi, moja.
32 Na upande wa mashariki, elfu nne na mia tano, kwa kupima; na malango matatu; lango la Yusufu, moja; lango la Benyamini, moja; lango la Dani, moja.
33 Na upande wa kusini, elfu nne na mia tano kwa kupima; na malango matatu; lango la Simeoni, moja; lango la Isakari, moja; lango la Zabuloni, moja.
34 Na upande wa magharibi, elfu nne na mia tano; pamoja na malango yake matatu; lango la Gadi, moja; lango la Asheri, moja; na lango la Naftali, moja.
35 Kuuzunguka ni mianzi kumi na nane elfu; na jina la mji huo tangu siku hiyo litakuwa hili, Bwana yupo hapa.