0:00
0:00

Mlango 46

Neno la Bwana lililomjia Yeremia, nabii, katika habari za mataifa.
2 Katika habari za Misri; habari za jeshi la Farao Neko, mfalme wa Misri, lililokuwa karibu na mto Frati katika Karkemishi, ambalo Nebukadreza, mfalme wa Babeli, alilipiga katika mwaka wa nne wa Yehoyakimu, mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda.
3 Tengenezeni kigao na ngao, mkakaribie ili kupigana.
4 Watandikeni farasi; pandeni, enyi mpandao farasi; simameni na chapeo zenu, isugueni mikuki; zivaeni dirii.
5 Nimeyaona haya kwa sababu gani? Wamefadhaika, wamerudi nyuma; mashujaa wao wamevunjika-vunjika; wanakimbia upesi sana, hawatazami nyuma; hofu ziko pande zote; asema Bwana.
6 Mtu mwepesi asikimbie, wala shujaa asiokoke; pande za kaskazini karibu na mto Frati wamejikwaa na kuanguka.
7 Nani huyu ajiinuaye kama mto Nile, Ambaye maji yake yanajirusha kama mito?
8 Misri anajiinua kama mto Nile, Na maji yake yanajirusha kama mito; Asema, Nitajiinua, nitaifunikiza nchi; Nitauharibu mji na hao wakaao ndani yake.
9 Haya! Pandeni, enyi farasi; Jihimizeni, enyi magari ya vita; Mashujaa nao na watoke nje Kushi na Puti, watumiao ngao; Nao Waludi, washikao uta na kuupeta.
10 Maana hiyo ni siku ya Bwana, Bwana wa majeshi, Siku ya kisasi, ili ajilipize kisasi juu ya adui zake; Nao upanga utakula na kushiba, Utakunywa damu yao hata kukinai; Maana Bwana, Bwana wa majeshi, ana sadaka yake Katika nchi ya kaskazini karibu na mto Frati.
11 Panda uende Gileadi, ukatwae zeri, Ee binti, bikira wa Misri; unatumia dawa nyingi bure tu; hupati kupona kamwe.
12 Mataifa wamesikia habari za aibu yako, nayo dunia imejaa kilio chako; maana shujaa amejikwaa juu ya shujaa mwenzake, wameanguka wote wawili pamoja.
13 Neno hili ndilo ambalo Bwana alimwambia Yeremia, nabii, kueleza jinsi Nebukadreza, mfalme wa Babeli, atakavyokuja na kuipiga nchi ya Misri.
14 Tangazeni habari hii katika Misri, mkaihubiri katika Migdoli, na kuihubiri katika Nofu, na Tahpanesi; semeni, Simama, ujifanye tayari kwa maana upanga umekula pande zako zote.
15 Mbona mashujaa wako wamechukuliwa mbali? Hawakusimama kwa sababu Bwana aliwafukuza.
16 Aliwakwaza wengi, naam, wakaangukiana wao kwa wao; wakasema, Haya! Na tuondoke, tukarudi kwa watu wetu wenyewe, hata nchi tuliyozaliwa, tuukimbie upanga unaotuonea.
17 Wakalia huko, Farao, mfalme wa Misri, ni kishindo tu; muhula alioandikiwa ameuacha upite.
18 Kama mimi niishivyo, asema Mfalme, ambaye jina lake ni Bwana wa majeshi, hakika yake, kama Tabori katika milima, na kama Karmeli karibu na bahari, ndivyo atakavyokuja.
19 Ee binti ukaaye katika Misri, Ujiweke tayari kwenda zako hali ya kufungwa; Kwa maana Nofu utakuwa ukiwa, Utateketezwa, usikaliwe na watu.
20 Misri ni mtamba mzuri sana, lakini uharibifu umekuja, Umekuja utokao pande za kaskazini.
21 Na watu wake waliojiwa, walio kati yake, Ni kama ndama waliowanda malishoni; Maana wao nao wamerudi nyuma, Wamekimbia wote pamoja, wasisimame; Maana siku ya msiba wao imewafikilia, Wakati wa kujiliwa kwao.
22 Sauti yake ni kama nyoka, wajapo kwa nguvu, Watamjia na mashoka, kama wachanja kuni.
23 Wataukata msitu wake, asema Bwana, ingawa haupenyeki; Kwa maana ni wengi kuliko nzige, hawahesabiki.
24 Binti ya Misri ataaibishwa; Atatiwa mikononi mwa watu wa kaskazini.
25 Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Tazama, nitamwadhibu Amoni wa No, na Farao, na Misri, pamoja na miungu yake, na wafalme wake, naam, Farao, na hao wanaomtumainia;
26 nami nitawatia katika mikono ya hao wanaowatafuta roho zao, na katika mikono ya Nebukadreza, mfalme wa Babeli, na katika mikono ya watumishi wake; na baada ya hayo itakaliwa na watu, kama katika siku za kale, asema Bwana.
27 Lakini usiogope wewe, Ee Yakobo, mtumishi wangu; wala usifadhaike, Ee Israeli; kwa maana, tazama, nitakuokoa toka mbali, na wazao wako toka nchi ya uhamisho wao; na Yakobo atarudi, naye atatulia na kustarehe, wala hapana mtu atakayemtia hofu.
28 Usiogope wewe, Ee Yakobo, mtumishi wangu, asema Bwana; kwa maana mimi ni pamoja nawe; maana nitawakomesha kabisa mataifa yote huko nilikokufukuza, bali sitakukomesha wewe kabisa; lakini nitakurudi kwa hukumu, wala sitakuacha bila adhabu.