0:00
0:00

Mlango 21

Neno hili ndilo lililomjia Yeremia, kutoka kwa Bwana, hapo mfalme Sedekia alipompelekea Pashuri, mwana wa Malkiya, na Sefania, mwana wa Maaseya, kuhani, kusema,
2 Tafadhali utuulizie habari kwa Bwana; kwa maana Nebukadreza, mfalme wa Babeli, analeta vita juu yetu; labda Bwana atatutendea sawasawa na kazi zake zote za ajabu, ili aende zake akatuache.
3 Basi Yeremia akawaambia, Mwambieni Sedekia neno hili,
4 Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi, Angalieni, nitazigeuza nyuma silaha za vita zilizo mikononi mwenu, ambazo kwa hizo ninyi mnapigana na mfalme wa Babeli, na Wakaldayo, wanaowahusuru nje ya kuta zenu, nami nitazikusanya pamoja katikati ya mji huu.
5 Na mimi mwenyewe nitapigana nanyi, kwa mkono ulionyoshwa na kwa mkono hodari, naam, kwa hasira, na kwa ukali, na kwa ghadhabu nyingi.
6 Nami nitawapiga wenyeji wa mji huu, wanadamu na wanyama pia; watakufa kwa tauni kubwa.
7 Na baada ya hayo, asema Bwana, nitamtia Sedekia, mfalme wa Yuda, na watumishi wake, na watu wote waliosalia ndani ya mji huu, baada ya tauni ile, na upanga, na njaa, katika mkono wa Nebukadreza, mfalme wa Babeli, na katika mikono ya adui zao, na katika mikono ya watu wale wanaowatafuta roho zao; naye atawaua kwa ukali wa upanga; hatawaachilia, wala hatawahurumia, wala hatawarehemu.
8 Nawe waambie watu hawa, Bwana asema hivi, Tazama naweka mbele yenu njia ya uzima, na njia ya mauti.
9 Yeye atakayekaa katika mji huu atakufa kwa upanga, na kwa njaa, na kwa tauni; bali yeye atakayetoka, na kujitia pamoja na Wakaldayo wanaowahusuru, yeye ataishi, na maisha yake yatakuwa nyara kwake.
10 Maana nimeweka uso wangu juu ya mji huu niuletee mabaya, wala nisiuletee mema, asema Bwana; utatiwa katika mkono wa mfalme wa Babeli, naye atauteketeza.
11 Na katika habari za nyumba ya mfalme wa Yuda, lisikieni neno la Bwana,
12 Ee nyumba ya Daudi, Bwana asema hivi, Hukumuni hukumu ya haki asubuhi, mkawaponye waliotekwa nyara na mkono wake aliyewadhulumu, ghadhabu yangu isije ikatoka kama moto, ikaunguza, asiweze mtu ye yote kuuzima, kwa sababu ya uovu wa matendo yenu.
13 Tazama, mimi ni juu yako, Ewe ukaaye bondeni, na kwenye jabali la uwandani, asema Bwana ninyi mnaosema, Ni nani atakayeshuka apigane nasi? Au, Ni nani atakayeingia katika makao yetu?
14 Nami nitawaadhibu kwa kadiri ya matunda ya matendo yenu, asema Bwana; nami nitawasha moto katika msitu wake, nao utateketeza vitu vyote viuzungukavyo.