0:00
0:00

Mlango 10

Enyi nyumba ya Israeli, lisikieni neno awaambialo Bwana;
2 Bwana asema hivi, Msijifunze njia ya mataifa, wala msishangae kwa sababu ya ishara za mbinguni; maana mataifa hushangaa kwa sababu ya ishara hizo.
3 Maana desturi za watu hao ni ubatili, maana mtu mmoja hukata mti mwituni, kazi ya mikono ya fundi na shoka.
4 Huupamba kwa fedha na dhahabu; huukaza kwa misumari na nyundo, usitikisike.
5 Mfano wao ni mfano wa mtende, kazi ya cherehani, hawasemi; hawana budi kuchukuliwa, kwa sababu hawawezi kwenda. Usiwaogope; kwa maana hawawezi kutenda uovu, wala hawana uwezo wa kutenda mema.
6 Hapana hata mmoja aliye kama wewe, Ee Bwana; wewe ndiwe uliye mkuu, na jina lako ni kuu katika uweza.
7 Ni nani asiyekucha wewe, Ee mfalme wa mataifa? Maana hii ni sifa yako wewe; kwa kuwa miongoni mwa wenye hekima wote wa mataifa, na katika hali yao ya enzi yote pia, hapana hata mmoja kama wewe.
8 Lakini wote pia huwa kama wanyama, ni wapumbavu. Haya ni maelezo ya sanamu, ni shina la mti tu.
9 Iko fedha iliyofuliwa ikawa mabamba, iliyoletwa kutoka Tarshishi, na dhahabu kutoka Ufazi, kazi ya stadi na ya mikono ya mfua dhahabu; mavazi yao ni rangi ya samawi na urujuani; hayo yote ni kazi ya mafundi yao.
10 Bali Bwana ndiye Mungu wa kweli; Ndiye Mungu aliye hai, Mfalme wa milele; Mbele za ghadhabu yake nchi yatetemeka, Wala mataifa hawawezi kustahimili hasira yake.
11 Mtawaambia hivi, Miungu hiyo isiyofanya mbingu na nchi, hiyo itaangamia katika nchi, nayo itatoweka chini ya mbingu.
12 Ameiumba dunia kwa uweza wake, Ameuthibitisha ulimwengu kwa hekima yake, Na kwa ufahamu wake amezitandika mbingu.
13 Atoapo sauti yake, pana mshindo wa maji mbinguni, Naye hupandisha mawingu toka ncha za nchi; Huifanyia mvua umeme, Huutoa upepo katika hazina zake.
14 Kila mtu amekuwa kama mnyama, hana maarifa; Kila mfua dhahabu amefedheheshwa na sanamu yake ya kuchonga; Maana sanamu yake ya kuyeyuka ni uongo, Wala hamna pumzi ndani yake.
15 Ni ubatili tu, ni kazi za udanganyifu; Wakati wa kujiliwa kwao watapotea.
16 Yeye, Fungu la Yakobo, siye kama hawa; Maana ndiye aliyeviumba vitu vyote; Na Israeli ni kabila ya urithi wake; Bwana wa majeshi ndilo jina lake.
17 Haya! Kusanya bidhaa yako katika nchi, wewe ukaaye katika mazingiwa.
18 Maana Bwana asema hivi, Tazama, wakati huu nitawatupa wenyeji wa nchi hii kama kwa kombeo, nitawataabisha, wapate kuona taabu.
19 Ole wangu, kwa sababu ya jeraha yangu! Pigo langu laumia; lakini nalisema, Kweli, ni huzuni yangu mimi, nami sina budi kuivumilia.
20 Hema yangu umetekwa nyara, kamba zangu zote zimekatika; watoto wangu wameniacha na kwenda zao, pia hawako. Hapana mtu atakayenitandikia tena hema yangu, na kuyatundika mapazia yangu.
21 Kwa sababu wachungaji wamekuwa kama wanyama, wala hawakuuliza kwa Bwana; basi hawakufanikiwa, na makundi yao yote yametawanyika.
22 Sauti imesikiwa, Tazama, inakuja; mshindo mkuu kutoka nchi ya kaskazini, ili kuifanya miji ya Yuda kuwa ukiwa, makao ya mbweha.
23 Ee Bwana, najua ya kuwa njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.
24 Ee Bwana, unirudi kwa haki; si kwa hasira yako, usije ukaniangamiza.
25 Hasira yako uwamwagie mataifa wasiokujua, na jamaa zao wasioliitia jina lako; kwa maana wamemla Yakobo, naam, wamemla kabisa na kumwangamiza, na kuyafanya makao yake kuwa ukiwa.