0:00
0:00

Mlango 29

Maneno haya ndiyo maneno ya waraka, ambao nabii Yeremia aliupeleka toka Yerusalemu, kwa hao waliobaki wa wakuu waliochukuliwa mateka, na kwa makuhani, na kwa manabii, na kwa watu wote, ambao Nebukadreza aliwachukua mateka toka Yerusalemu hata Babeli;
2 (hapo walipokwisha kutoka Yerusalemu Yekonia mfalme, na mama yake mfalme, na matowashi, na wakuu wa Yuda na Yerusalemu, na mafundi, na wahunzi;)
3 kwa mkono wa Elasa, mwana wa Shafani, na Gemaria, mwana wa Hilkia, (ambao Sedekia, mfalme wa Yuda, aliwatuma hata Babeli, kwa Nebukadreza, mfalme wa Babeli), kusema,
4 Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, awaambia hivi watu wote waliochukuliwa mateka, niliowafanya wachukuliwe toka Yerusalemu mpaka Babeli;
5 Jengeni nyumba, mkakae ndani yake, kapandeni bustani, mkale matunda yake;
6 oeni wake, mkazae wana na binti; kawaozeni wake wana wenu, mkawaoze waume binti zenu, wazae wana na binti; mkaongezeke huko wala msipungue.
7 Kautakieni amani mji ule, ambao nimewafanya mchukuliwe mateka, mkauombee kwa Bwana; kwa maana katika amani yake mji huo ninyi mtapata amani.
8 Maana Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Manabii walio kati yenu, na wabashiri wenu, wasiwadanganye ninyi, wala msisikilize ndoto zenu, mnazootesha.
9 Kwa maana kwa jina langu hutabiri maneno ya uongo kwenu; mimi sikuwatuma, asema Bwana.
10 Maana Bwana asema hivi, Babeli utakapotimiziwa miaka sabini, nitawajilia ninyi, na kulitimiza neno langu jema kwenu, kwa kuwarudisha mahali hapa.
11 Maana nayajua mawazo ninayowawazia ninyi, asema Bwana, ni mawazo ya amani wala si ya mabaya, kuwapa ninyi tumaini siku zenu za mwisho.
12 Nanyi mtaniita, mtakwenda na kuniomba, nami nitawasikiliza.
13 Nanyi mtanitafuta na kuniona, mtakaponitafuta kwa moyo wenu wote.
14 Nami nitaonekana kwenu, asema Bwana, nami nitawarudisha watu wenu waliofungwa, nami nitawakusanya ninyi, nikiwatoa katika mataifa yote, na katika mahali pote, nilikowafukuza, asema Bwana; nami nitawaleta tena, hata mahali ambapo kutoka hapo naliwafanya mchukuliwe mateka.
15 Maana mmesema, Bwana ametuinulia manabii huko Babeli.
16 Maana Bwana asema hivi, katika habari za mfalme aketiye katika kiti cha enzi cha Daudi, na katika habari za watu wote wakaao ndani ya mji huu, ndugu zenu wasiokwenda pamoja nanyi kufungwa;
17 Bwana wa majeshi asema hivi, Tazama, nitaleta juu yao upanga, na njaa, na tauni, nami nitawafanya kuwa kama tini mbovu, zisizoweza kuliwa, kwa kuwa ni mbovu sana.
18 Nami nitawafuatia kwa upanga, na njaa, na tauni, nami nitawatoa watupwe huko na huko katika falme zote za dunia, wawe kitu cha kulaaniwa, na cha kushangaza, na cha kuzomewa, na cha kulaumiwa, katika mataifa yote nilikowafukuza.
19 Kwa sababu hawakusikiliza maneno yangu, asema Bwana, ambayo naliwatuma watumishi wangu, hao manabii, nikiamka mapema, na kuwatuma; lakini hamkutaka kusikiliza, asema Bwana.
20 Basi, lisikieni neno la Bwana, ninyi nyote mliochukuliwa mateka, niliowapeleka toka Yerusalemu mpaka Babeli.
21 Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, katika habari za Ahabu, mwana wa Kolaya, na katika habari za Sedekia, mwana wa Maaseya, wawatabiriao ninyi maneno ya uongo kwa jina langu; Tazama, nitawatia katika mikono ya Nebukadreza, mfalme wa Babeli, naye atawaua mbele ya macho yenu.
22 Tena katika habari zao laana itatumiwa na wafungwa wote wa Yuda, walioko Babeli, kusema, Bwana akufanye uwe kama Sedekia, na kama Ahabu, ambao mfalme wa Babeli aliwaoka motoni;
23 kwa sababu wametenda upumbavu katika Israeli, nao wamezini na wake za jirani zao, nao wamenena maneno ya uongo kwa jina langu, nisiyowaamuru; nami ndimi nijuaye, nami ni shahidi, asema Bwana.
24 Na katika habari za Shemaya, Mnehelami, utanena, ukisema,
25 Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, ya kwamba, Kwa kuwa kwa jina lako mwenyewe umewapelekea barua watu wote walioko Yerusalemu, na Sefania, mwana wa Maaseya, kuhani, na makuhani wote, kusema,
26 Bwana amekufanya kuhani badala ya Yehoyada, kuhani, ili mpate kuwa watumishi katika nyumba ya Bwana, kwa kila mtu aliye na wazimu, na kwa kila mtu ajifanyaye kuwa nabii, umtie katika mkatale na pingu.
27 Mbona, basi, hukumkemea Yeremia wa Anathothi, ajifanyaye kuwa nabii kwenu,
28 ambaye ametuma watu kwetu katika Babeli, kusema, Uhamisho huu ni wa siku nyingi; jengeni nyumba, mkakae ndani yake; pandeni bustani, mkale matunda yake.
29 Na Sefania, kuhani, akasoma barua hii masikioni mwa Yeremia nabii.
30 Ndipo neno la Bwana likamjia Yeremia, kusema,
31 Uwapelekee habari watu wote waliohamishwa, kusema, Bwana asema hivi, katika habari za Shemaya, Mnehelami; Kwa sababu Shemaya amewatabiria ninyi, lakini sikumtuma mimi, naye amewatumainisha neno la uongo;
32 basi, Bwana asema hivi, Tazama, nitamwadhibu Shemaya, Mnehelami, na wazao wake; hatakuwa na mtu atakayekaa katika watu hawa, wala hatayaona mema nitakayowatendea watu wangu, asema Bwana; kwa sababu amenena maneno ya uasi juu ya Bwana.