0:00
0:00

Mlango 22

Heri kuchagua jina jema kuliko mali nyingi; Na neema kuliko fedha na dhahabu.
2 Tajiri na maskini hukutana pamoja; Bwana ndiye aliyewaumba wote wawili.
3 Mwenye busara huyaona mabaya na kujificha; Bali wajinga huendelea mbele wakaumia.
4 Thawabu ya unyenyekevu ambao ni kumcha Bwana Ni utajiri, na heshima, nayo ni uzima.
5 Miiba na mitego huwa katika njia ya mshupavu; Yeye aitunzaye nafsi yake atakuwa mbali nayo.
6 Mlee mtoto katika njia impasayo, Naye hataiacha, hata atakapokuwa mzee.
7 Tajiri humtawala maskini, Naye akopaye ni mtumwa wake akopeshaye.
8 Yeye apandaye uovu atavuna msiba, Na fimbo ya ghadhabu yake itakoma.
9 Mwenye jicho la ukarimu atabarikiwa; Maana huwapa maskini chakula chake.
10 Mtupe nje mwenye dharau, na ugomvi utatoka; Naam, fitina na fedheha zitakoma.
11 Apendaye usafi wa moyo, na neema ya midomo; Mfalme atakuwa rafiki yake.
12 Macho ya Bwana humhifadhi mwenye maarifa; Bali huyapindua maneno ya mtu haini.
13 Mtu mvivu husema, Simba yuko nje; Nitauawa katika njia kuu.
14 Kinywa cha malaya ni shimo refu; Anayechukiwa na Bwana atatumbukia ndani yake.
15 Ujinga umefungwa ndani ya moyo wa mtoto; Lakini fimbo ya adhabu itaufukuzia mbali.
16 Yeye awaoneaye maskini ili kuongeza mapato, Naye ampaye tajiri, hupata hasara.
17 Tega sikio lako uyasikie maneno ya wenye hekima, na kuuelekeza moyo wako kwa maarifa yangu;
18 maana ni vizuri kuyahifadhi ndani yako, hali yakithibitika pamoja midomoni mwako.
19 Ili matumaini yako uyaweke kwa Bwana, leo nimekujulisha wewe haya, naam, wewe.
20 Je! Sikukuandikia mambo makuu juu ya mashauri na juu ya maarifa;
21 ili kukujulisha hakika ya maneno ya kweli, uwarudishie wakutumao maneno ya kweli?
22 Usimnyang'anye maskini, kwa kuwa ni maskini; Wala usimdhulumu mtu mnyonge langoni;
23 Kwa sababu Bwana atawatetea; Naye atawateka uhai wao waliowateka.
24 Usifanye urafiki na mtu mwenye hasira nyingi; Wala usiende na mtu wa ghadhabu nyingi;
25 Usije ukajifunza njia zake; Na kujipatia nafsi yako mtego.
26 Usiwe mmoja wao wawekao rehani; Au walio wadhamini kwa deni za watu;
27 Kama huna kitu cha kulipa; Kwani ukaondolee kitanda chako chini yako?
28 Usiiondoe alama ya mpaka wa zamani, Uliowekwa na baba zako.
29 Je! Wamwona mtu mwenye bidii katika kazi zake? Huyo atasimama mbele ya wafalme; Hatasimama mbele ya watu wasio na cheo.