0:00
0:00

Mlango 32

Basi hao watu watatu wakaacha kumjibu Ayubu, kwa sababu alikuwa mwenye haki machoni pake mwenyewe.
2 Ndipo zikawaka hasira za huyo Elihu mwana wa Barakeli, Mbuzi, katika jamaa ya Ramu, juu ya Ayubu, kwa sababu alikuwa amejipa haki mwenyewe zaidi ya Mungu.
3 Tena hasira zake ziliwaka juu ya hao rafiki zake watatu kwa sababu hawakupata jawabu, lakini wamemhukumia Ayubu makosa.
4 Basi huyo Elihu alikuwa anangoja ili anene na Ayubu, kwa sababu hao wengine walikuwa wazee kuliko yeye.
5 Hata Elihu alipoona kuwa hapana jawabu katika vinywa vya watu hao watatu, hasira zake ziliwaka.
6 Basi Elihu mwana wa Barakeli, Mbuzi, akajibu, na kusema, Mimi ni kijana, na ninyi ni wazee sana; Kwa hiyo nilijizuia, nisithubutu kuwaonyesha nionavyo.
7 Nilisema, Yafaa siku ziseme, Na wingi wa miaka ufundishe hekima.
8 Lakini imo roho ndani ya mwanadamu, Na pumzi za Mwenyezi huwapa akili.
9 Sio wakuu walio wenye akili, Wala sio wazee watambuao hukumu.
10 Basi nilisema, Nisikilizeni mimi; Mimi nami nitawaonyesha nionavyo.
11 Tazama, niliyangojea maneno yenu, Nilizisikiliza nisikie hoja zenu, Hapo mlipokitafuta mtakalonena.
12 Naam, niliwasikiza ninyi, Na tazama, hapana mmoja aliyemshinda Ayubu, Wala kumjibu maneno yake, kati yenu.
13 Jitunzeni msiseme, Sisi tumepata hekima; Mungu yumkini akamshinda, si mtu;
14 Kwa kuwa yeye hajayaelekeza maneno yake kwangu; Wala sitamjibu mimi kwa maneno yenu.
15 Wameshangaa, hawajibu tena; Hawana neno la kusema.
16 Na mimi, je! Ningoje, kwa sababu hawaneni, Kwa sababu wasimama kimya, wala wasijibu tena;
17 Mimi nami nitajibu sehemu yangu, Mimi nami nitaonyesha nionavyo.
18 Kwa kuwa nimejaa maneno; Roho iliyo ndani yangu hunihimiza.
19 Tazama, tumbo langu ni kama divai iliyozibwa; Kama viriba vipya li karibu na kupasuka.
20 Nitanena, ili nipate kutulia; Nitafunua midomo yangu na kujibu.
21 Tafadhali, nisiupendelee uso wa mtu; Wala sitajipendekeza kwa mtu ye yote.
22 Kwani mimi sijui kujipendekeza; Au Muumba wangu angeniondoa kwa upesi.