0:00
0:00

Mlango 34

Yosia alikuwa na umri wa miaka minane alipoanza kutawala; akatawala miaka thelathini na mmoja huko Yerusalemu.
2 Akafanya yaliyo mema machoni pa Bwana, akaziendea njia za Daudi babaye, asigeuke kwa kuume wala kwa kushoto.
3 Kwa kuwa katika mwaka wa nane wa kutawala kwake, naye akali mchanga, alianza kumtafuta Mungu wa Daudi babaye; hata katika mwaka wa kumi na mbili akaanza kusafisha Yuda na Yerusalemu kwa kuondoa mahali pa juu, na kwa kuondoa maashera, na sanamu za kuchora, nazo za kusubu.
4 Wakazibomoa madhabahu za mabaali machoni pake; na sanamu za jua, zilizoinuliwa juu yake, akazikata-kata; na maashera, na sanamu za kuchonga, nazo za kusubu, akazivunja-vunja, akaziponda kuwa mavumbi, akayamimina juu ya makaburi ya hao waliozichinjia dhabihu.
5 Akaiteketeza mifupa ya makuhani madhabahuni mwao, akasafisha Yuda na Yerusalemu.
6 Na katika miji ya Manase, na Efraimu, na Simeoni, mpaka Naftali, akafanya vile vile; na katika maganjo yake pande zote.
7 Akazibomoa madhabahu, akaponda-ponda maashera na sanamu kuwa mavumbi, akazikata-kata sanamu zote za jua katika nchi yote ya Israeli, kisha akarejea Yerusalemu.
8 Hata katika mwaka wa kumi na nane wa kutawala kwake, alipokwisha kuisafisha nchi, na nyumba, akamtuma Shafani, mwana wa Azalia, na Maaseya, akida wa mji, na Yoa, mwana wa Yoahazi, mwandishi wa tarehe, waitengeneze nyumba ya Bwana, Mungu wake.
9 Wakamjia Hilkia kuhani mkuu, wakampa fedha, iliyoletwa nyumbani mwa Mungu, waliyoikusanya Walawi, wangoje mlango, mikononi mwa Manase na Efraimu, na mabaki yote ya Israeli, na Yuda yote na Benyamini, na wenyeji wa Yerusalemu.
10 Wakaitia mikononi mwa watenda kazi walioisimamia nyumba ya Bwana; na hao mafundi waliotenda kazi nyumbani mwa Bwana wakaitoa kwa kuitengeneza na kuifanya upya nyumba;
11 wakawapa maseremala na waashi, ili wanunue mawe ya kuchonga, na miti ya kuungia, na kuifanyiza boriti kwa nyumba zile walizoziharibu wafalme wa Yuda.
12 Nao watu wakatenda kazi kwa uaminifu; na wasimamizi wao walikuwa Yahathi na Obadia, Walawi, wa wana wa Merari; na Zekaria na Meshulamu, wa wana wa Wakohathi, ili kuihimiza kazi; na wengine katika Walawi, wote waliokuwa wastadi wa kupiga vinanda.
13 Tena walikuwa juu ya wachukuzi wa mizigo, wakawahimiza wote waliotenda kazi ya huduma yo yote; na miongoni mwa Walawi kulikuwa na waandishi, na wasimamizi, na mabawabu.
14 Nao walipotoa ile fedha iliyoletwa nyumbani mwa Bwana, Hilkia kuhani akakiona kitabu cha torati ya Bwana iliyotolewa kwa mkono wa Musa.
15 Akajibu Hilkia akamwambia Shafani mwandishi, Kitabu cha torati nimekiona nyumbani mwa Bwana. Hilkia akampa Shafani kile kitabu.
16 Shafani akampelekea mfalme hicho kitabu, tena akampasha mfalme habari, akisema, Yote waliyokabidhiwa watumishi wako, wayafanya.
17 Nao wameimimina fedha iliyoonekana nyumbani mwa Bwana, nayo wameitia mikononi mwa wasimamizi, na mikononi mwa watenda kazi.
18 Shafani mwandishi akamweleza mfalme, akisema, Hilkia kuhani amenipa kitabu. Shafani akasoma ndani yake mbele ya mfalme.
19 Ikawa, mfalme alipoyasikia maneno ya torati, aliyararua mavazi yake.
20 Mfalme akawaamuru Hilkia, na Ahikamu, mwana wa Shafani, na Abdoni, mwana wa Mika, na Shafani mwandishi, na Asaya, mtumishi wa mfalme, kusema,
21 Nendeni, mkamwulize Bwana kwa ajili yangu, na kwa hao waliosalia wa Israeli na wa Yuda, katika habari za maneno ya kitabu kilichoonekana; maana ghadhabu ya Bwana ni nyingi iliyomwagika juu yetu, kwa sababu baba zetu hawakulishika neno la Bwana, kutenda sawasawa na yote yaliyoandikwa kitabuni humo.
22 Basi Hilkia, na hao waliotumwa na mfalme, wakamwendea Hulda nabii mke, mkewe Shalumu, mwana wa Tohathi, mwana wa Hasra, mtunza mavazi; (naye alikuwa akikaa Yerusalemu katika mtaa wa pili); wakasema naye kama hayo.
23 Akawaambia, Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi; Mwambieni mtu huyo aliyewatuma kwangu,
24 Bwana asema hivi, Angalia, nitaleta mabaya juu ya mahali hapa, na juu ya wakaao, laana zote zilizoandikwa katika kitabu hicho walichokisoma mbele ya mfalme wa Yuda;
25 kwa sababu wameniacha mimi, na kuifukizia uvumba miungu mingine, ili wanikasirishe mimi kwa matendo yote ya mikono yao; kwa hiyo ghadhabu yangu imemwagika juu ya mahali hapa, wala isizimike.
26 Lakini mfalme wa Yuda, aliyewatuma kumwuliza Bwana, mtamwambia hivi, Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi; Kwa habari ya maneno uliyoyasikia,
27 kwa kuwa moyo wako ulikuwa mwororo, nawe umejinyenyekeza mbele ya Mungu, uliposikia maneno yake juu ya mahali hapa, na juu ya wakaao, ukajinyenyekeza mbele zangu, na kuyararua mavazi yako, na kulia mbele zangu; mimi nami nimekusikia, asema Bwana.
28 Tazama, nitakukusanya kwa baba zako, nawe utawekwa kaburini mwako kwa amani, wala macho yako hayataona mabaya yote nitakayoyaleta juu ya mahali hapa, na juu ya wakaao. Basi wakamrudishia mfalme habari.
29 Ndipo mfalme akapeleka wajumbe, akawakusanya wazee wote wa Yuda na Yerusalemu.
30 Akapanda mfalme nyumbani kwa Bwana, na watu wote wa Yuda, na wenyeji wa Yerusalemu, na makuhani na Walawi, na watu wote, wakubwa kwa wadogo; naye akasoma masikioni mwao maneno yote ya kitabu cha agano kilichoonekana nyumbani mwa Bwana.
31 Akasimama mfalme mahali pake, akafanya agano mbele za Bwana, kumfuata Bwana, na kuzishika amri zake, na shuhuda zake, na sheria zake, kwa moyo wake wote, na kwa roho yake yote, kuyatenda maneno ya agano yaliyoandikwa kitabuni humo.
32 Akawafanya wote walioonekana katika Yerusalemu na Benyamini walikubali. Na wenyeji wa Yerusalemu wakafanya sawasawa na agano la Mungu, Mungu wa baba zao.
33 Naye Yosia akayaondolea mbali machukizo yote katika nchi zote zilizokuwa milki ya wana wa Israeli, akawafanya wote walioonekana katika Israeli kutumika, naam, wamtumikie Bwana, Mungu wao. Siku zake zote hawakuacha kumfuata Bwana, Mungu wa baba zao.