0:00
0:00

Mlango 31

Basi Wafilisti wakapigana na Israeli; nao watu wa Israeli wakakimbia mbele ya Wafilisti, wakaanguka wameuawa katika mlima wa Gilboa.
2 Wafilisti wakamfuatia sana Sauli na wanawe, Wafilisti wakawaua Yonathani, na Abinadabu, na Malkishua, wana wa Sauli.
3 Tena vita vilikuwa vikali sana juu ya Sauli, na wapiga upinde wakampata; hata akafadhaika sana kwa sababu ya wapiga upinde.
4 Ndipo Sauli akamwambia yule mchukua silaha zake, Futa upanga wako, unichome nao; wasije watu hawa wasiotahiriwa wakanichoma, na kunisimanga. Lakini huyo mchukua silaha zake akakataa; kwa sababu aliogopa sana. Basi Sauli akautwaa upanga wake, akauangukia.
5 Na mchukua silaha zake alipoona ya kuwa Sauli amekufa, yeye naye akauangukia upanga wake, akafa pamoja naye.
6 Hivyo Sauli akafa, na wanawe watatu, na mchukua silaha zake, na watu wake wote pamoja siku iyo hiyo.
7 Kisha watu wa Israeli waliokuwa upande wa pili wa bonde lile, na ng'ambo ya Yordani, walipoona ya kuwa watu wa Israeli wamekimbia, na ya kuwa Sauli na wanawe wamekufa, wakaiacha miji yao, wakakimbia; nao Wafilisti wakaenda wakakaa humo.
8 Hata ikawa, siku ya pili yake, Wafilisti walipokwenda kuwateka nyara waliouawa, walimwona Sauli na wanawe watatu wameanguka juu ya mlima wa Gilboa.
9 Wakamkata kichwa, wakamvua silaha zake, wakapeleka wajumbe kwenda nchi ya Wafilisti pande zote, ili kutangaza habari nyumbani mwa sanamu zao, na kwa watu.
10 Wakaziweka silaha zake nyumbani mwa Maashtorethi; wakakitundika kiwiliwili chake katika ukuta wa Beth-shani.
11 Na wenyeji wa Yabesh-Gileadi waliposikia habari zake, jinsi hao Wafilisti walivyomtenda Sauli,
12 wakainuka mashujaa wote, wakaenda usiku kucha, wakautwaa mwili wake Sauli, na miili ya wanawe, na kuiondoa ukutani kwa Beth-shani nao wakaja Yabeshi, na kuiteketeza huko.
13 Kisha wakaitwaa mifupa yao, na kuizika chini ya mkwaju huko Yabeshi, nao wakafunga siku saba.