0:00
0:00

Mlango 9

Kisha Bwana akanena na Musa katika bara ya Sinai, mwezi wa kwanza wa mwaka wa pili baada ya kutoka kwao katika nchi ya Misri, akamwambia,
2 Tena, wana wa Israeli na washike sikukuu ya Pasaka kwa wakati wake ulioagizwa.
3 Siku ya kumi na nne ya mwezi huu, wakati wa jioni, mtaishika kwa wakati wake ulioagizwa; kwa amri zake zote, na kama hukumu zake zote zilivyo, ndivyo mtakavyoishika.
4 Kisha Musa akawaambia wana wa Israeli kwamba waishike sikukuu hiyo ya Pasaka;
5 Nao wakaishika Pasaka katika mwezi wa kwanza, siku ya kumi na nne ya mwezi, wakati wa jioni, katika bara ya Sinai vile vile kama hayo yote Bwana aliyomwagiza Musa, ndivyo walivyofanya wana wa Israeli.
6 Basi walikuwako watu waume kadha wa kadha waliokuwa na unajisi kwa ajili ya maiti wa mtu, hata wasiweze kuishika Pasaka siku hiyo; nao wakaenda mbele ya Musa na Haruni, siku hiyo hao watu wakamwambia,
7 Sisi tu hali ya unajisi kwa ajili ya maiti wa mtu; nasi tumezuiwa kwa nini hata tusipate kumtolea Bwana matoleo kwa wakati wake ulioagizwa, kati ya wana wa Israeli?
8 Musa akawaambia, Ngojeni hapo; hata nipate sikiza Bwana atakaloagiza juu yenu.
9 Bwana akanena na Musa, akamwambia,
10 Nena na wana wa Israeli, kuwaambia, Mtu wa kwenu, au wa vizazi vyenu, ye yote atakayekuwa na unajisi kwa ajili ya maiti, au akiwako mbali katika safari, na haya yote, ataishika Pasaka kwa Bwana;
11 mwezi wa pili, siku ya kumi na nne ya mwezi, wakati wa jioni, wataishika; watamla pamoja na mikate isiyotiwa chachu na mboga za uchungu;
12 wasisaze kitu chake cho chote hata asubuhi, wala wasimvunje mfupa wake; kama hiyo sheria yote ya Pasaka ilivyo ndivyo watakavyoishika.
13 Lakini mtu aliye safi, wala hakuwa katika safari, naye amekosa kuishika Pasaka, mtu huyo atakatiliwa mbali na watu wake; kwa sababu hakumtolea Bwana matoleo kwa wakati wake ulioamriwa, mtu huyo atachukua dhambi yake.
14 Na kama mgeni akiketi kati yenu ugenini, naye ataka kuishika Pasaka kwa Bwana; kama hiyo sheria ya Pasaka ilivyo, na kama amri yake ilivyo, ndivyo atakavyofanya; mtakuwa na sheria moja, kwa huyo aliye mgeni, na kwa huyo aliyezaliwa katika nchi.
15 Na siku hiyo maskani iliposimamishwa, lile wingu likaifunika maskani, yaani, hema ya kukutania; wakati wa jioni likawa juu ya maskani, mfano wa moto, hata asubuhi.
16 Ndivyo ilivyokuwa sikuzote; lile wingu liliifunika kwa mfano wa moto usiku.
17 Na kila lilipoinuliwa lile wingu juu ya ile Hema ndipo wana wa Israeli waliposafiri; na mahali lilipokaa lile wingu, ndipo wana wa Israeli walipopiga kambi yao.
18 Kwa amri ya Bwana Wana wa Israeli walisafiri, na kwa amri ya Bwana walipiga kambi; wakati lile wingu ilipokaa juu ya maskani walikaa katika kambi yao.
19 Na lile wingu lilipokawia juu ya maskani siku nyingi, ndipo wana wa Israeli walipolinda malinzi ya Bwana, wala hawakusafiri.
20 Na pengine lile wingu lilikaa juu ya maskani siku chache; ndipo kwa amri ya Bwana walikaa katika kambi yao, tena kwa amri ya Bwana walisafiri.
21 Na pengine lile wingu lilikaa tangu jioni hata asubuhi; na lile wingu lilipoinuliwa asubuhi walisafiri, au kama likikaa usiku na mchana pia, lilipoinuliwa lile wingu, ndipo waliposafiri.
22 Ikiwa lile wingu lilikawia, likikaa juu ya maskani siku mbili, au mwezi, au mwaka, wana wa Israeli walikaa katika kambi yao, wasisafiri;
23 bali lilipoinuliwa walisafiri. Kwa amri ya Bwana walipiga kambi yao, na kwa amri ya Bwana walisafiri; wakayalinda malinzi ya Bwana, kwa mkono wa Musa.