0:00
0:00

Mlango 15

Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia,
2 Nena na wana wa Israeli, na kuwaambia, Mtakapoingia nchi yenu ya kukaa, niwapayo,
3 nanyi mwataka kumsongezea Bwana sadaka kwa moto, kwamba ni sadaka ya kuteketezwa, au dhabihu ya kuchinjwa, ili kuondoa nadhiri, au kuwa sadaka ya hiari, au katika sikukuu zenu zilizoamriwa, ili kumfanyia Bwana harufu ipendezayo, katika ng'ombe, au katika kondoo;
4 ndipo yeye atakayetoa matoleo yake na amtolee Bwana sadaka ya unga ya sehemu ya kumi ya efa ya unga mwembamba uliochanganywa na robo ya hini ya mafuta;
5 na divai kwa sadaka ya kinywaji, robo ya hini, utaiandaa pamoja na sadaka ya kuteketezwa, au kwa dhabihu ya kuchinjwa, kwa ajili ya kila mwana-kondoo.
6 Au kwa ajili ya kondoo mume, utaiandaa sadaka ya unga ya sehemu za kumi mbili za efa ya unga mwembamba uliochanganywa na sehemu ya tatu ya hini ya mafuta;
7 na kwa sadaka ya kinywaji utasongeza sehemu ya tatu ya hini ya divai, kuwa harufu ya kupendeza kwa Bwana.
8 Tena hapo utakapomwandaa ng'ombe mume kwa sadaka ya kuteketezwa, au kwa dhabihu ya kuchinjwa, kwa kuondoa nadhiri, au kwa sadaka za amani kwa Bwana;
9 ndipo utakapotoa, pamoja na huyo ng'ombe, sadaka ya unga ya sehemu za kumi tatu za efa ya unga mwembamba uliochanganywa na nusu ya hini ya mafuta.
10 Tena utasongeza nusu ya hini ya divai kwa sadaka ya kinywaji, kwa sadaka iliyosongezwa kwa moto, ya harufu ya kupendeza kwa Bwana.
11 Ndivyo itakavyofanywa kwa kila ng'ombe, au kwa kila kondoo mume, au kwa kila mwana-kondoo mume, au kila mwana-mbuzi.
12 Kama hesabu ilivyo ya hao mtakaowaandaa, ndivyo mtakavyofanya kwa kila mmoja, sawasawa na hesabu yao.
13 Wote ambao wamezaliwa kwenu watafanya hayo yote kwa kuandama mfano huo, katika kusongeza sadaka kwa moto, ya harufu ya kupendeza kwa Bwana.
14 Tena kwamba mgeni amekaa kwenu, au mtu ye yote aliye kati yenu katika vizazi vyenu, naye yuataka kusongeza sadaka kwa moto, na harufu ya kupendeza kwa Bwana; kama ninyi mfanyavyo, na yeye atafanya vivyo.
15 Katika huo mkutano, kutakuwa na amri moja kwenu ninyi na kwa mgeni akaaye pamoja nanyi; ni amri ya milele katika vizazi vyenu; kama ninyi mlivyo, na mgeni atakuwa vivyo mbele za Bwana.
16 Itakuwa sheria moja na amri moja kwenu ninyi na kwa mgeni akaaye nanyi.
17 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia,
18 Nena na wana wa Israeli, uwaambie, Mtakapoingia nchi niwapelekayo,
19 ndipo itakapokuwa ya kwamba hapo mtakapokula katika chakula cha nchi hiyo, mtamsongezea Bwana sadaka ya kuinuliwa.
20 Katika unga wenu wa kwanza wa chenga-chenga mtasongeza mkate uwe sadaka ya kuinuliwa; vile vile kama mfanyavyo sadaka ya kuinuliwa ya sakafu ya kupuria nafaka, ndivyo mtakavyoiinua.
21 Malimbuko ya unga wenu mtampa Bwana sadaka ya kuinuliwa, katika vizazi vyenu.
22 Tena mtakapokosa, msiyashike maagizo hayo yote Bwana aliyomwambia Musa,
23 hayo yote Bwana aliyowaagiza kwa mkono wa Musa, tangu siku hiyo Bwana aliyoleta maagizo, na baadaye katika vizazi vyenu
24 ndipo itakapokuwa, kama ni kosa lililofanywa pasipo kujua, wala mkutano haukuwa na fahamu, ndipo mkutano wote utasongeza ng'ombe mume mmoja mdogo kuwa sadaka ya kuteketezwa, kuwa harufu ya kupendeza kwa Bwana, pamoja na sadaka yake ya unga, na sadaka yake ya kinywaji, kama amri ilivyo, na mbuzi mume mmoja kuwa sadaka ya dhambi.
25 Naye kuhani atafanya upatanisho kwa ajili ya mkutano wote wa wana wa Israeli, nao watasamehewa; maana, lilikuwa ni kosa, nao wamekwisha leta matoleo yao, sadaka iliyosongezwa kwa Bwana kwa moto, na sadaka yao ya dhambi pia wameileta mbele za Bwana kwa ajili ya kosa lao;
26 nao mkutano wote wa wana wa Israeli watasamehewa, na mgeni akaaye kati yao; maana, katika habari za hao wote jambo hilo lilitendeka pasipo kujua.
27 Tena kama mtu mmoja akifanya dhambi pasipo kujua, ndipo atasongeza mbuzi mmoja mke wa mwaka wa kwanza kuwa sadaka ya dhambi.
28 Naye kuhani atafanya upatanisho kwa ajili ya huyo mtu akosaye, atakapofanya dhambi pasipo kujua, mbele za Bwana, ili kufanya upatanisho kwa ajili yake; naye atasemehewa.
29 Mtakuwa na sheria moja kwa huyo afanyaye neno lo lote pasipo kujua, kwa huyo aliyezaliwa kwenu kati ya wana wa Israeli, na kwa mgeni akaaye kati yao.
30 Lakini mtu afanyaye neno lo lote kwa kusudi, kama ni mzalia, kama ni mgeni, huyo amtukana Bwana; na mtu huyo atakatiliwa mbali na watu wake.
31 Kwa sababu amelidharau neno la Bwana, na kuyavunja maagizo yake; mtu huyo atakatiliwa mbali, uovu wake utakuwa juu yake.
32 Kisha wakati huo wana wa Israeli walipokuwako jangwani, wakamwona mtu mmoja akikusanya kuni siku ya Sabato.
33 Hao waliomwona akikusanya kuni wakamleta kwa Musa na Haruni, na kwa mkutano wote.
34 Nao wakamweka kifungoni, maana, lilikuwa halijasemwa atakalotendwa.
35 Bwana akamwambia Musa, Mtu huyo lazima atauawa; mkutano wote watampiga kwa mawe huko nje ya marago.
36 Basi mkutano wote wakampeleka nje ya marago, nao wakampiga kwa mawe, akafa; kama Bwana alivyomwagiza Musa.
37 Kisha Bwana akasema na Musa, na kumwambia,
38 Nena na wana wa Israeli, na kuwaagiza ya kwamba wajifanyie vishada katika ncha za nguo zao, katika vizazi vyao, tena ya kwamba watie katika kila kishada cha kila ncha nyuzi za rangi ya samawi;
39 nacho kitakuwa kwenu ni kishada, ili mpate kukiangalia, na kuyakumbuka maagizo yote ya Bwana, na kuyafanya; tena kwamba msiende kutanga-tanga kuandama mioyo yenu wenyewe, na macho yenu wenyewe, ambayo mlikuwa mkiyaandama kwa uasherati hapo kwanza;
40 ili mpate kukumbuka na kuyafanya maagizo yangu yote, na kuwa watakatifu kwa Mungu wenu.
41 Mimi ndimi Bwana, Mungu wenu, niliyewaleta kutoka nchi ya Misri, ili kwamba niwe Mungu wenu; mimi ndimi Bwana, Mungu wenu.