0:00
0:00

Mlango 29

Tena mwezi wa saba, siku ya kwanza ya mwezi, mtakuwa na kusanyiko takatifu; hamtafanya kazi yo yote ya utumishi; ni siku ya kupiga tarumbeta kwenu.
2 Nanyi mtasongeza sadaka ya kuteketezwa kuwa harufu ya kupendeza kwa Bwana; ng'ombe mume mdogo mmoja, na kondoo mume mmoja, na wana-kondoo waume wa mwaka wa kwanza wakamilifu saba;
3 pamoja na sadaka yake ya unga, unga mwembamba uliochanganywa na mafuta, sehemu ya kumi tatu kwa ng'ombe, sehemu ya kumi mbili kwa kondoo mume,
4 na sehemu ya kumi moja kwa kila mwana-kondoo katika wale wana-kondoo saba;
5 na mbuzi mume mmoja kuwa sadaka ya dhambi, ili kufanya upatanisho kwa ajili yenu;
6 zaidi ya hiyo sadaka ya kuteketezwa ya kuandama mwezi, na sadaka yake ya unga, na hiyo sadaka ya kuteketezwa ya sikuzote, na sadaka yake ya unga, na sadaka zake za vinywaji, kama ilivyo amri yake, kuwa harufu ya kupendeza, ni sadaka iliyosongezwa kwa Bwana kwa moto.
7 Tena siku ya kumi ya huo mwezi wa saba mtakuwa na kusanyiko takatifu; nanyi mtazitesa nafsi zenu, msifanye kazi yo yote ya utumishi
8 lakini mtamsongezea Bwana sadaka ya kuteketezwa, kuwa harufu ya kupendeza; ng'ombe mume mdogo mmoja, na kondoo mume mmoja, na wana-kondoo waume wa mwaka wa kwanza saba; watakuwa wakamilifu kwenu;
9 pamoja na sadaka zake za unga, unga mwembamba uliochanganywa na mafuta, sehemu ya kumi tatu kwa huyo ng'ombe, na sehemu ya kumi mbili kwa huyo kondoo,
10 na sehemu ya kumi moja kwa kila mwana-kondoo katika wale wana-kondoo saba;
11 na mbuzi mume mmoja kuwa sadaka ya dhambi; zaidi ya hiyo sadaka ya dhambi ya upatanisho, na hiyo sadaka ya kuteketezwa ya sikuzote, na sadaka yake ya unga, na sadaka zake za vinywaji.
12 Tena siku ya kumi na tano ya mwezi wa saba mtakuwa na kusanyiko takatifu; hamtafanya kazi yo yote ya utumishi, nanyi mtamfanyia Bwana sikukuu muda wa siku saba;
13 nanyi mtasongeza sadaka ya kuteketezwa, sadaka isongezwayo kwa moto, harufu ya kupendeza kwa Bwana; ng'ombe waume wadogo kumi na watatu, na kondoo waume wawili, na wana-kondoo waume wa mwaka wa kwanza kumi na wanne; wote watakuwa wakamilifu;
14 pamoja na sadaka zake za unga, unga mwembamba uliochanganywa na mafuta, sehemu ya kumi tatu kwa kila ng'ombe katika wale kumi na watatu na sehemu ya kumi mbili kwa kila kondoo katika hao kondoo waume wawili;
15 na sehemu ya kumi moja kwa kila mwana-kondoo katika wale wana-kondoo kumi na wanne;
16 na mbuzi mume mmoja kuwa sadaka ya dhambi zaidi ya hiyo sadaka ya kuteketezwa ya sikuzote, na sadaka yake ya unga, na sadaka yake ya kinywaji.
17 Tena siku ya pili mtasongeza ng'ombe waume wadogo kumi na wawili, na kondoo waume wawili, na wana-kondoo waume wa mwaka wa kwanza kumi na wanne wakamilifu;
18 pamoja na sadaka yake ya unga, na sadaka zake za vinywaji kwa hao ng'ombe, na kwa hao kondoo, na kwa wale wana-kondoo, kama hesabu yao ilivyo, kwa kuandama hiyo amri;
19 na mbuzi mume mmoja kuwa sadaka ya dhambi; zaidi ya hiyo sadaka ya kuteketezwa ya sikuzote, na sadaka yake ya unga, na sadaka zake za vinywaji.
20 Tena siku ya tatu mtasongeza ng'ombe waume kumi na mmoja, na kondoo waume wawili, na wana-kondoo waume wa mwaka wa kwanza wakamilifu kumi na wanne;
21 pamoja na sadaka yake ya unga, na sadaka zake za vinywaji, kwa hao ng'ombe, na kwa hao kondoo, na kwa wale wana-kondoo, kama hesabu yao ilivyo, kwa kuiandama amri;
22 na mbuzi mume mmoja kuwa sadaka ya dhambi; zaidi ya hiyo sadaka ya kuteketezwa ya sikuzote, na sadaka yake ya unga, na sadaka yake ya kinywaji.
23 Tena siku ya nne mtasongeza ng'ombe waume kumi, na kondoo waume wawili, na wana-kondoo waume wa mwaka wa kwanza wakamilifu kumi na wanne;
24 na sadaka yake ya unga, na sadaka zake za vinywaji kwa hao ng'ombe, na kwa hao kondoo, na kwa wale wana-kondoo, kama hesabu yao ilivyo, kwa kuiandama amri;
25 na mbuzi mume mmoja kuwa sadaka ya dhambi, zaidi ya hiyo sadaka ya kuteketezwa ya sikuzote, na sadaka yake ya unga, na sadaka yake ya kinywaji.
26 Tena siku ya tano mtasongeza ng'ombe waume kenda, na kondoo Waume wawili, na wana-kondoo waume wa mwaka wa kwanza wakamilifu kumi na wanne;
27 pamoja na sadaka yake ya unga, na sadaka zake za vinywaji, kwa hao ng'ombe, na kwa hao kondoo, na kwa wale wana-kondoo, kama hesabu yao ilivyo, kwa kuiandama amri;
28 na mbuzi mume mmoja kuwa sadaka ya dhambi; zaidi ya hiyo sadaka ya kuteketezwa ya siku zote, na hiyo sadaka yake ya unga na sadaka yake ya kinywaji.
29 Tena siku ya sita mtasongeza ng'ombe waume wanane, na kondoo waume wawili, na wana-kondoo waume wa mwaka wa kwanza wakamilifu kumi na wanne;
30 pamoja na sadaka yake ya unga, na sadaka zake za vinywaji, kwa hao ng'ombe, na kwa hao kondoo, na kwa wale wana-kondoo, kama hesabu yao ilivyo, kwa kuiandama amri;
31 na mbuzi mume mmoja kuwa sadaka ya dhambi; zaidi ya hiyo sadaka ya kuteketezwa ya siku zote, na hiyo sadaka yake ya unga na sadaka yake ya kinywaji.
32 Tena siku ya saba mtasongeza ng'ombe waume saba, na kondoo waume wawili, na wana-kondoo waume wa mwaka wa kwanza wakamilifu kumi na wanne;
33 pamoja na sadaka yake ya unga, na sadaka zake za vinywaji, kwa hao ng'ombe, na kwa hao kondoo, na kwa wale wana-kondoo, kama hesabu yao ilivyo, kwa kuiandama amri;
34 na mbuzi mume mmoja kuwa sadaka ya dhambi; zaidi ya hiyo sadaka ya kuteketezwa ya siku zote, na hiyo sadaka yake ya unga na sadaka yake ya kinywaji.
35 Tena siku ya nane mtakuwa na kusanyiko la makini sana; hamtafanya kazi yo yote ya utumishi;
36 lakini mtasongeza sadaka ya kuteketezwa, sadaka ya kusongezwa kwa moto, harufu ya kupendeza kwa Bwana; ng'ombe mume mmoja, na kondoo mume mmoja, na wana-kondoo waume wa mwaka wa kwanza wakamilifu saba;
37 pamoja na sadaka yake ya unga, na sadaka zake za vinywaji, kwa huyo ng'ombe, na kwa huyo kondoo mume, na kwa wale wana-kondoo, kama hesabu yao ilivyo, kwa kuiandama amri;
38 na mbuzi mume mmoja kuwa sadaka ya dhambi; zaidi ya hiyo sadaka ya kuteketezwa ya siku zote, na hiyo sadaka yake ya unga na sadaka yake ya kinywaji.
39 Sadaka hizo mtamsongezea Bwana katika sikukuu zenu zilizoamriwa, zaidi ya nadhiri zenu, na sadaka zenu za hiari, kuwa sadaka zenu za kuteketezwa, na sadaka zenu za unga, na sadaka zenu za vinywaji, na sadaka zenu za amani.
40 Naye Musa akawaambia wana wa Israeli vile vile kama hayo yote Bwana alivyomwagiza Musa.