Maombolezo

1 2 3 4 5

0:00
0:00

Mlango 5

Ee Bwana, kumbuka yaliyotupata; Utazame na kuiona aibu yetu.
2 Urithi wetu umegeuka kuwa mali ya wageni; Na nyumba zetu kuwa mali ya makafiri.
3 Tumekuwa yatima waliofiwa na baba; Mama zetu wamekuwa kama wajane.
4 Tumekunywa maji yetu kwa fedha; Kuni zetu twauziwa.
5 Watufuatiao wa juu ya shingo zetu; Tumechoka tusipate raha yo yote.
6 Tumewapa hao Wamisri mkono; Na Waashuri nao, ili tushibe chakula.
7 Baba zetu walitenda dhambi hata hawako; Na sisi tumeyachukua maovu yao.
8 Watumwa wanatutawala; Hakuna mtu wa kutuokoa na mikono yao.
9 Twapata chakula kwa kujihatarisha nafsi zetu; Kwa sababu ya upanga wa nyikani.
10 Ngozi yetu ni nyeusi kama tanuu; Kwa sababu ya hari ya njaa ituteketezayo.
11 Huwatia jeuri wanawake katika Sayuni; Na mabikira katika miji ya Yuda.
12 Wakuu hutungikwa kwa mikono yao; Nyuso za wazee hazipewi heshima.
13 Vijana huyachukua mawe ya kusagia; Na watoto hujikwaa chini ya kuni.
14 Wazee wameacha kwenda langoni; Na vijana kwenda ngomani.
15 Furaha ya mioyo yetu imekoma; Machezo yetu yamegeuka maombolezo.
16 Taji ya kichwa chetu imeanguka; Ole wetu! Kwa kuwa tumetenda dhambi.
17 Kwa sababu hiyo mioyo yetu imezimia; Kwa ajili ya hayo macho yetu hayaoni vema.
18 Kwa ajili ya mlima Sayuni ulio ukiwa, Mbweha hutembea juu yake.
19 Wewe, Bwana, unadumu milele; Kiti chako cha enzi ni tangu kizazi hata kizazi.
20 Mbona watusahau sikuzote; Na kutuacha muda huu mwingi?
21 Ee Bwana, utugeuze kwako, nasi tutageuka; Zifanye mpya siku zetu kama siku za kale.
22 Isipokuwa wewe umetukataa kabisa; Nawe una hasira nyingi sana juu yetu.