Maombolezo

1 2 3 4 5

0:00
0:00

Mlango 4

Jinsi dhahabu ilivyoacha kung'aa, Na dhahabu iliyo safi ilivyobadilika! Mawe ya patakatifu yametupwa Mwanzo wa kila njia.
2 Wana wa Sayuni wenye thamani, Walinganao na dhahabu safi, Jinsi wanavyodhaniwa kuwa vyombo vya udongo, Kazi ya mikono ya mfinyanzi!
3 Hata mbwa-mwitu hutoa matiti, Huwanyonyesha watoto wao; Binti ya watu wangu amekuwa mkali, Mfano wa mbuni jangwani.
4 Ulimi wa mtoto anyonyaye Wagandamana na kaakaa lake kwa kiu; Watoto wachanga waomba chakula, Wala hakuna hata mmoja awamegeaye.
5 Wale waliokula vitu vya anasa Wameachwa peke yao njiani; Wale waliokuzwa kuvaa nguo nyekundu Wakumbatia jaa.
6 Maana uovu wa binti ya watu wangu ni mkubwa Kuliko dhambi ya Sodoma, Uliopinduliwa kama katika dakika moja, Wala mikono haikuwekwa juu yake.
7 Wakuu wake walikuwa safi kuliko theluji, Walikuwa weupe kuliko maziwa; Miili yao, walikuwa wekundu kuliko marijani, Na umbo lao kama yakuti samawi.
8 Nyuso zao ni nyeusi kuliko makaa; Hawajulikani katika njia kuu; Ngozi yao yagandamana na mifupa yao Imekauka, imekuwa kama mti.
9 Heri wale waliouawa kwa upanga Kuliko wao waliouawa kwa njaa; Maana hao husinyaa, wakichomwa Kwa kukosa matunda ya mashamba.
10 Mikono ya wanawake wenye huruma Imewatokosa watoto wao wenyewe; Walikuwa ndio chakula chao Katika uharibifu wa binti ya watu wangu.
11 Bwana ameitimiza kani yake, Ameimimina hasira yake kali; Naye amewasha moto katika Sayuni Ulioiteketeza misingi yake.
12 Wafalme wa dunia hawakusadiki, Wala wote wakaao duniani, Ya kwamba mtesi na adui wangeingia Katika malango ya Yerusalemu.
13 Ni kwa sababu ya dhambi za manabii wake Na maovu ya makuhani wake, Walioimwaga damu ya wenye haki Katikati yake.
14 Hutanga-tanga njiani kama vipofu, Wametiwa unajisi kwa damu; Hata ikawa watu wasiweze Kuyagusa mavazi yao.
15 Watu waliwapigia kelele, Ondokeni, Uchafu, Ondokeni, ondokeni, msiguse; Walipokimbia na kutanga-tanga, watu walisema kati ya mataifa, Hawatakaa hapa tena.
16 Hasira ya Bwana imewatenga, Yeye hatawaangalia tena; Hawakujali nafsi za wale makuhani, Hawakuwaheshimu wazee wao.
17 Macho yetu yamechoka Kwa kuutazamia bure msaada wetu; Katika kungoja kwetu tumengojea taifa Lisiloweza kutuokoa.
18 Wanatuvizia hatua zetu, Hata hatuwezi kwenda katika njia zetu; Mwisho wetu umekaribia, siku zetu zimetimia; Maana mwisho wetu umefika.
19 Waliotufuatia ni wepesi Kuliko tai za mbinguni; Hao walitufuatia milimani, Nao walituotea jangwani.
20 Pumzi ya mianzi ya pua zetu, masihi wa BWANA, Alikamatwa katika marima yao;Ambaye kwa habari zake tulisema,Chini ya kivuli chake tukakaa kati ya mataifa.
21 Furahi, ushangilie, Ee binti Edomu, Ukaaye katika nchi ya Usi; Hata kwako kikombe kitapita, Utalewa, na kujifanya uchi.
22 Uovu wako umetimia, Ee binti Sayuni; Hatakuhamisha tena; Atapatiliza uovu wako, Ee binti Edomu; Atazivumbua dhambi zako.