0:00
0:00

Mlango 7

Na sheria ya hiyo sadaka ya hatia ni hii; ni takatifu sana.
2 Wataichinja sadaka ya hatia pale pale waichinjapo sadaka ya kuteketezwa; na damu yake atainyunyiza katika madhabahu pande zote.
3 Katika sadaka hiyo atasongeza mafuta yake yote; yaani, mkia wake wenye mafuta, na mafuta yafunikayo matumbo,
4 na figo zake mbili, na mafuta yaliyoshikamana nazo, yaliyo karibu na kiuno chake, na kitambi kilicho katika ini, pamoja na figo zake mbili, hayo yote atayaondoa;
5 na kuhani atayateketeza juu ya madhabahu, kuwa dhabihu kwa Bwana kwa njia ya moto; ni sadaka ya hatia.
6 Kila mtu mume miongoni mwa makuhani atakula katika sadaka hiyo; italiwa katika mahali patakatifu; ni takatifu sana.
7 Kama hiyo sadaka ya dhambi ilivyo, na sadaka ya hatia ni vivyo; sheria yake ni moja; huyo kuhani afanyaye upatanisho kwayo, ndiye atakayekuwa nayo.
8 Tena kuhani atakayesongeza sadaka ya kuteketezwa ya mtu awaye yote, huyo kuhani atatwaa awe nayo ngozi ya huyo mnyama wa sadaka ya kuteketezwa aliyemsongeza.
9 Na kila sadaka ya unga iliyookwa mekoni, na yote yaliyoandaliwa chunguni, au kaangoni, yote yatakuwa ya huyo kuhani aliyeyasongeza.
10 Na kila sadaka ya unga, kama umeandaliwa na mafuta, au kama ni mkavu, watautwaa wana wote wa Haruni kuutumia, kila mtu sawasawa.
11 Na sheria ya matoleo ya sadaka za amani, atakazosongeza mtu kwa Bwana, ni hii.
12 Kwamba aitoa kwa ajili ya shukrani, ndipo atakaposongeza pamoja na hiyo sadaka ya shukrani mikate isiyotiwa chachu, iliyoandaliwa na mafuta, na mikate ya kaki isiyochachwa iliyopakwa mafuta, na mikate ya unga mwembamba uliolowama mafuta.
13 Ataleta matoleo yake, pamoja na mikate iliyotiwa chachu, na pamoja na sadaka zake za amani, kwa ajili ya shukrani.
14 Na katika hayo atasongeza kimoja katika kila toleo kiwe sadaka ya kuinuliwa kwa Bwana; itakuwa ni ya kuhani atakayeinyunyiza hiyo damu ya sadaka za amani.
15 Na hiyo nyama ya sadaka zake za amani zilizochinjwa kwa ajili ya shukrani italiwa siku iyo hiyo ya matoleo yake; asisaze yo yote hata asubuhi.
16 Lakini kwamba hii sadaka ya matoleo yake ni nadhiri, au sadaka ya hiari, italiwa siku hiyo aliyoileta sadaka yake; kisha siku ya pili yake kitakachosalia kitaliwa;
17 lakini hicho kitakachosalia, katika hizo nyama za sadaka, hata siku ya tatu kitachomwa moto.
18 Tena kama nyama yo yote katika hiyo dhabihu yake ya sadaka za amani ikiliwa siku ya tatu, haitakubaliwa, wala haitahesabiwa kwake huyo mwenye kuisongeza; itakuwa ni machukizo, na mtu atakayeila atachukua uovu wake.
19 Tena nyama itakayogusa kitu kilicho najisi haitaliwa; itachomwa moto. Na katika hiyo nyama nyingine, kila mtu aliye safi ana ruhusa kuila;
20 lakini mtu huyo atakayekula katika nyama ya sadaka za amani, ambazo ni za Bwana, na unajisi wake akiwa nao juu yake, mtu huyo atakatiliwa mbali na watu wake.
21 Kisha mtu awaye yote atakapogusa kitu cho chote kilicho najisi, uchafu wa binadamu, au mnyama aliye najisi, au machukizo yo yote yaliyo najisi, kisha akala nyama ya dhabihu ya sadaka za amani, ambazo ni za Bwana, mtu huyo atakatiliwa mbali na watu wake.
22 Bwana akanena na Musa, na kumwambia,
23 Nena na wana wa Israeli, uwaambie, Msile mafuta yo yote, ya ng'ombe, wala ya kondoo, wala ya mbuzi.
24 Tena mafuta ya mnyama afaye mwenyewe, na mafuta ya mnyama aliyeraruliwa na wanyama, mna ruhusa kuyatumia kwa ajili ya matumizi mengine; lakini msiyale kabisa.
25 Kwani huyo mtu atakayekula mafuta ya mnyama, ambaye ni katika wanyama ambao watu husongeza sadaka kwa Bwana kwa moto, mtu huyo atakayekula mafuta hayo atakatiliwa mbali na watu wake.
26 Tena msiile damu yo yote, ama ya ndege, ama ya mnyama, katika nyumba zenu zote.
27 Mtu ye yote alaye damu, mtu huyo atakatiliwa mbali na watu wake.
28 Bwana akanena na Musa, na kumwambia,
29 Nena na wana wa Israeli uwaambie, Yeye asongezaye dhabihu yake ya sadaka za amani kwa Bwana, atamletea Bwana matoleo yake, kutoka katika ile dhabihu ya sadaka zake za amani;
30 mikono yake mwenyewe itamletea hizo sadaka za kusongezwa kwa moto; mafuta yake pamoja na kidari atayaleta, ili kwamba hicho kidari kitikiswe kuwa sadaka ya kutikiswa mbele ya Bwana.
31 Kuhani atayateketeza hayo mafuta juu ya madhabahu; lakini hicho kidari kitakuwa cha Haruni na cha wanawe.
32 Mguu wa nyuma wa upande wa kuume mtampa kuhani kuwa sadaka ya kuinuliwa kutoka katika hizo sadaka zenu za amani.
33 Katika wana wa Haruni, huyo atakayeisongeza damu ya sadaka za amani, na mafuta yake, yeye atapata mguu wa nyuma wa upande wa kuume kuwa sehemu yake.
34 Kwa maana, hicho kidari cha kutikiswa, na huo mguu wa kuinuliwa, nimevitwaa kwa wana wa Israeli, katika dhabihu zao za sadaka za amani, nami nimempa Haruni kuhani na wanawe, kuwa haki yao ya milele kutoka kwa wana wa Israeli.
35 Hii ndiyo sehemu ya Haruni, na sehemu ya wanawe, katika kutiwa mafuta kwao, katika hizo dhabihu zisongezwazo kwa Bwana kwa njia ya moto, siku hiyo aliyowaweka ili wamtumikie Bwana katika kazi ya ukuhani;
36 sehemu ambayo Bwana aliagiza wapewe na wana wa Israeli, siku hiyo aliyowatia mafuta. Ni haki yao ya milele katika vizazi vyao vyote.
37 Sheria ya sadaka ya kuteketezwa ni hii, na ya sadaka ya unga, na ya sadaka ya dhambi, na ya sadaka ya hatia, na ya kuwekwa wakfu, na ya sadaka za amani;
38 ambazo Bwana alimwagiza Musa katika mlima wa Sinai, siku hiyo aliyowaagiza wana wa Israeli wamtolee Bwana matoleo yao, huko katika jangwa la Sinai.