0:00
0:00

Mlango 37

Kisha Bezaleli akalifanya lile sanduku la mti wa mshita, urefu wake ulikuwa dhiraa mbili na nusu, na upana wake ulikuwa dhiraa moja na nusu, na kwenda juu kwake kulikuwa ni dhiraa moja na nusu;
2 akalifunika dhahabu safi, ndani na nje, akafanya na ukingo wa dhahabu kulizunguka pande zote.
3 Naye akasubu pete nne za dhahabu kwa ajili yake, katika miguu yake minne; pete mbili upande wake mmoja na pete mbili upande wake wa pili.
4 Akafanya na miti ya kulichukulia, ya mti wa mshita akaifunika dhahabu.
5 Naye akaitia hiyo miti katika zile pete zilizokuwa ubavuni mwa sanduku, ili kulichukua hilo sanduku.
6 Kisha akafanya kiti cha rehema cha dhahabu safi; urefu wake ulikuwa dhiraa mbili na nusu na upana wake ulikuwa dhiraa moja na nusu.
7 Kisha akafanya makerubi mawili ya dhahabu; akayafanya ya kazi ya kufua, yawe katika miisho miwili ya kiti cha rehema;
8 kerubi moja mwisho huu, na kerubi moja mwisho huu; alifanya hayo makerubi mawili ya kitu kimoja na hicho kiti cha rehema katika miisho yake miwili.
9 Na hayo makerubi yakayanyosha mabawa yao juu, na kukifunika hicho kiti cha rehema kwa mabawa yao, na nyuso zao zilikuwa zaelekeana hili na hili; nyuso za hayo makerubi zilikuwa zikielekea kiti cha rehema.
10 Kisha akafanya hiyo meza ya mti wa mshita; urefu wake ulikuwa ni dhiraa mbili, na upana wake ulikuwa ni dhiraa moja, na kwenda juu kwake kulikuwa ni dhiraa moja na nusu;
11 naye akaifunika dhahabu safi, akaifanyia ukingo wa dhahabu kuizunguka pande zote.
12 Kisha akaifanyia upapi wa upana wa shibiri kuizunguka pande zote, akauzungushia ukingo wa urembo wa dhahabu ule upapi.
13 Naye akasubu vikuku vinne vya dhahabu kwa ajili yake, akavitia vile vikuku katika pembe nne, katika miguu yake minne.
14 Vile vikuku vilikuwa karibu na ule upapi, ili viwe mahali pa kutilia ile miti, ya kuichukulia meza.
15 Naye akaifanya hiyo miti ya kuichukulia, ya mti wa mshita, akaifunika dhahabu, ili kuichukua hiyo meza.
16 Kisha, vile vyombo vilivyokuwa juu ya meza, sahani zake, na miiko yake, na bakuli zake, na makopo yake ya kumiminia, akavifanya vya dhahabu safi.
17 Kisha akakifanya kile kinara cha taa cha dhahabu safi, akakifanya kile kinara cha taa cha kazi ya kufua, tako lake, na mti wake; vikombe vyake, na matovu yake, na maua yake, vyote vilikuwa vya kitu kimoja nacho,
18 nacho kilikuwa na matawi sita yaliyotoka ubavuni mwake; matawi matatu ya kinara yalikuwa upande huu, na matawi matatu ya kinara yalikuwa upande huu;
19 vikombe vitatu, vilivyofanywa mfano wa maua ya mlozi vilikuwa katika tawi moja, tovu na ua; na vikombe vitatu, vilivyofanywa mfano wa maua ya mlozi, katika tawi la pili, tovu na ua; yalikuwa ni vivyo hivyo yale matawi sita yaliyokuwa katika hicho kinara.
20 Katika kinara mlikuwa na vikombe vinne, vilivyofanywa mfano wa maua ya mlozi, matovu yake na maua yake;
21 kisha chini ya matawi mawili mlikuwa na tovu iliyokuwa ya kitu kimoja nacho, na chini ya matawi mawili mengine mlikuwa na tovu ya kitu kimoja nacho, tena chini ya matawi mawili hayo mengine mlikuwa na tovu ya kitu kimoja nacho; kwa ajili ya hayo matawi sita, yaliyotokana nacho.
22 Hayo matovu yake na matawi yake yalikuwa ya kitu kimoja nacho; kinara hicho kizima chote pia ni kazi moja ya kufua ya dhahabu safi.
23 Kisha akafanya taa zake saba, na makoleo yake, na visahani vyake, vya dhahabu safi.
24 Akakifanya cha talanta moja ya dhahabu safi, pamoja na vyombo vyake vyote.
25 Kisha akafanya hiyo madhabahu ya kufukizia uvumba ya mti wa mshita; urefu wake ulikuwa ni dhiraa moja, na upana wake ulikuwa ni dhiraa moja, ilikuwa mraba; na kwenda juu kwake kulikuwa ni dhiraa mbili; na pembe zake zilikuwa za kitu kimoja nayo.
26 Naye akaifunika dhahabu safi, upande wa juu, na mbavu zake pande zote, na hizo pembe zake; akaifanyia na ukingo wa dhahabu kuizunguka pande zote.
27 Naye akaifanyia vikuku viwili vya dhahabu na kuvitia chini ya ukingo wake, katika mbavu zake mbili, katika pande zake mbili, viwe ni mahali pa hiyo miti ya kuichukulia.
28 Kisha akafanya hiyo miti kwa mti wa mshita, na kuifunika dhahabu.
29 Kisha akayafanya hayo mafuta matakatifu ya kutiwa, na ule uvumba safi wa viungo vya manukato vizuri, kwa kuandama kazi ya mtengezaji manukato.