3 Yohana

1

0:00
0:00

Mlango 1

Mzee, kwa Gayo mpenzi, nimpendaye katika kweli.
2 Mpenzi naomba ufanikiwe katika mambo yote na kuwa na afya yako, kama vile roho yako ifanikiwavyo.
3 Maana nalifurahi mno walipokuja ndugu na kuishuhudia kweli yako, kama uendavyo katika kweli.
4 Sina furaha iliyo kuu kuliko hii, kusikia ya kwamba watoto wangu wanakwenda katika kweli.
5 Mpenzi, kazi ile ni ya uaminifu uwatendeayo hao ndugu na hao wageni nao,
6 waliokushuhudia upendo wako mbele ya kanisa; utafanya vizuri ukiwasafirisha kama ipasavyo kwa Mungu.
7 Kwa maana, kwa ajili ya Jina hilo, walitoka, wasipokee kitu kwa Mataifa.
8 Basi imetupasa sisi kuwakaribisha watu kama hao, ili tuwe watenda kazi pamoja na kweli.
9 Naliliandikia kanisa neno, lakini Diotrefe, apendaye kuwa wa kwanza kati yao, hatukubali.
10 Kwa hiyo, nikija, nitayakumbuka matendo yake atendayo, atoavyo upuzi juu yetu kwa maneno maovu; wala hatoshwi na hayo, ila yeye mwenyewe hawakaribishi hao ndugu, na wale watakao kuwakaribisha, huwazuia, na kuwatoa katika kanisa.
11 Mpenzi, usiuige ubaya, bali uige wema. Yeye atendaye mema ni wa Mungu, bali yeye atendaye mabaya hakumwona Mungu.
12 Demetrio ameshuhudiwa na watu wote, tena na ile kweli yenyewe. Nasi pia twashuhudia, nawe wajua ya kwamba ushuhuda wetu ni kweli.
13 Nalikuwa na mambo mengi ya kukuandikia, lakini sipendi kukuandikia kwa wino na kalamu.
14 Lakini nataraji kukuona karibu, nasi tutasema uso kwa uso. [15] Amani kwako. Rafiki zetu wakusalimu. Wasalimu hao rafiki zetu, kila mtu kwa jina lake.