0:00
0:00

Mlango 6

Ilimpendeza Dario kuweka juu ya ufalme maliwali mia na ishirini, wawe juu ya ufalme wote;
2 na juu yao akaweka wakubwa watatu, na Danielii alikuwa mmoja wao; ili maliwali hawa watoe hesabu kwao, mfalme asipate hasara.
3 Basi Danielii huyo alipata sifa kuliko wakubwa na maliwali, kwa kuwa roho bora ilikuwa ndani yake; naye mfalme akaazimu kumweka juu ya ufalme wote.
4 Basi mawaziri na maamiri wakatafuta sana kupata sababu za kumshitaki Danielii kwa habari za mambo ya ufalme; lakini hawakuweza kuona sababu wala kosa; kwa maana alikuwa mwaminifu, wala halikuonekana kosa wala hatia ndani yake.
5 Ndipo wale watu wakasema, Hatutapata sababu ya kumshitaki Danielii huyo, tusipoipata katika mambo ya sheria ya Mungu wake.
6 Basi wale mawaziri na maamiri wakakusanyika pamoja mbele ya mfalme, wakamwambia hivi, Mfalme Dario, uishi milele.
7 Mawaziri wote wa ufalme, na manaibu, na maamiri, na madiwani, na maliwali wamefanya shauri pamoja ili kuweka amri ya kifalme; na kupiga marufuku, ya kwamba mtu ye yote atakayeomba dua kwa Mungu awaye yote, au kwa mtu awaye yote, katika muda wa siku thelathini, ila kwako, Ee mfalme atatupwa katika tundu la simba.
8 Sasa, Ee mfalme, piga marufuku, ukatie sahihi maandiko haya, yasibadilike, kama ilivyo sheria ya Wamedi na Waajemi, isiyoweza kubadilika.
9 Basi mfalme Dario akayatia sahihi maandiko yale, na ile marufuku.
10 Hata Danielii, alipojua ya kuwa yale maandiko yamekwisha kutiwa sahihi, akaingia nyumbani mwake, (na madirisha katika chumba chake yalikuwa yamefunguliwa kukabili Yerusalemu;) akapiga magoti mara tatu kila siku, akasali, akashukuru mbele za Mungu wake, kama alivyokuwa akifanya tokea hapo.
11 Basi watu hao wakakusanyika pamoja, wakamwona Danielii akiomba dua, na kusihi mbele za Mungu wake.
12 Ndipo wakakaribia, wakasema mbele ya mfalme katika habari ya ile marufuku ya mfalme; Je! Hukuitia sahihi ile marufuku, ya kwamba kila mtu atakayeomba dua kwa Mungu awaye yote, au kwa mtu awaye yote, katika muda wa siku thelathini, ila kwako, Ee mfalme, atatupwa katika tundu la simba? Mfalme akajibu, akasema, Neno hili ni kweli, kama ilivyo sheria ya Wamedi na Waajemi isiyoweza kubadilika.
13 Basi wakajibu, wakasema mbele ya mfalme, Yule Danielii, aliye mmoja wa wana wa wale waliohamishwa wa Yuda, hakujali wewe, Ee mfalme, wala ile marufuku uliyoitia sahihi, bali aomba dua mara tatu kila siku.
14 Basi mfalme aliposikia maneno haya alikasirika sana, akakaza moyo wake ili kumponya Danielii; akajitaabisha kumwokoa hata jua likachwa.
15 Ndipo watu wale wakakusanyika pamoja mbele ya mfalme, wakamwambia mfalme, Ee mfalme, ujue ya kuwa ni sheria ya Wamedi na Waajemi, lisibadilike neno lo lote lililo marufuku, wala amri yo yote iliyowekwa na mfalme.
16 Basi mfalme akatoa amri, nao wakamleta Danielii, wakamtupa katika tundu la simba. Mfalme akanena, akamwambia Danielii, Mungu wako unayemtumikia daima, yeye atakuponya.
17 Likaletwa jiwe, likawekwa mdomoni mwa lile tundu; naye mfalme akalitia muhuri kwa muhuri yake mwenyewe, na kwa muhuri ya wakuu wake, lisibadilike neno lo lote katika habari za Danielii.
18 Kisha mfalme akaenda nyumbani kwake, akakesha usiku kucha, akafunga; na vinanda havikuletwa mbele yake; na usingizi wake ukampaa.
19 Asubuhi mfalme akaondoka mapema, akaenda kwa haraka mpaka penye lile tundu la simba.
20 Naye alipolikaribia lile tundu, akamlilia Danielii kwa sauti ya huzuni; mfalme akanena; akamwambia Danielii, Ee Danielii, mtumishi wa Mungu aliye hai, je! Mungu wako, unayemtumikia daima, aweza kukuponya na simba hawa?
21 Ndipo Danielii akamwambia mfalme, Ee mfalme, uishi milele.
22 Mungu wangu amemtuma malaika wake, naye ameyafumba makanwa ya simba, nao hawakunidhuru; kwa kuwa mbele zake mimi nalionekana kuwa sina hatia; tena, mbele yako, Ee mfalme, sikukosa neno.
23 Basi mfalme akafurahi sana, akaamuru wamtoe Danielii katika lile tundu. Ndipo Danielii akatolewa katika lile tundu, wala dhara lo lote halikuonekana mwilini mwake, kwa sababu alikuwa anamtumaini Mungu wake.
24 Mfalme akaamuru, nao wakawaleta wale watu waliomshitaki Danielii, wakawatupa katika tundu la simba, wao, na watoto wao, na wake zao; na wale simba wakawashinda wakaivunja mifupa yao vipande vipande, kabla hawajafika chini ya tundu.
25 Ndipo mfalme Dario akawaandikia watu wa kabila zote, na taifa zote, na lugha zote, waliokaa juu ya uso wa dunia; Amani na iongezeke kwenu.
26 Mimi naweka amri, ya kwamba katika mamlaka yote ya ufalme wangu watu watetemeke na kuogopa mbele za Mungu wa Danielii; maana yeye ndiye Mungu aliye hai, adumuye milele, na ufalme wake ni ufalme usioharibika, na mamlaka yake itadumu hata mwisho.
27 Yeye huponya na kuokoa, hutenda ishara na maajabu mbinguni na duniani, ndiye aliyemponya Danielii na nguvu za simba.
28 Basi Danielii huyo akafanikiwa katika enzi ya Dario, na katika enzi ya Koreshi, Mwajemi.