0:00
0:00

Mlango 22

Basi Daudi akamwambia Bwana maneno ya wimbo huu, siku ile Bwana alipomwokoa mikononi mwa adui zake zote, na mkononi mwa Sauli;
2 akasema, Bwana ndiye jabali langu, na ngome yangu, na mwokozi wangu, naam, wangu;
3 Mungu wa mwamba wangu, nitamwamini yeye; Ngao yangu, na pembe ya wokovu wangu, mnara wangu, na makimbilio yangu; Mwokozi wangu, waniokoa na jeuri.
4 Nitamwita Bwana astahiliye kusifiwa; Hivyo nitaokoka na adui zangu.
5 Maana mawimbi ya mauti yalinizunguka, Mafuriko ya uovu yakanitia hofu.
6 Kamba za kuzimu zilinizunguka; Mitego ya mauti ikanikabili.
7 Katika shida yangu nalimwita Bwana, Naam, nikamlalamikia Mungu wangu;
8 Ndipo nchi ilipotikisika na kutetemeka, Misingi ya mbinguni ikasuka-suka Na kutikisika, kwa sababu alikuwa na ghadhabu.
9 Kukapanda moshi kutoka puani mwake, Moto ukatoka kinywani mwake ukala; Makaa yakawashwa nao.
10 Aliziinamisha mbingu akashuka; Kukawa na giza kuu chini ya miguu yake.
11 Akapanda juu ya kerubi akaruka; Naam, alionekana juu ya mabawa ya upepo.
12 Akafanya giza hema zake za kumzunguka, Makusanyiko ya maji, mawingu makuu ya mbinguni.
13 Toka mwangaza uliokuwa mbele zake Makaa ya moto yakawashwa.
14 Bwana alipiga radi toka mbinguni, Naye Aliye juu akaitoa sauti yake.
15 Akapiga mishale, akawatawanya; Umeme, naye akawatapanya.
16 Ndipo ilipoonekana mikondo ya bahari, Misingi ya ulimwengu ikafichuliwa, Kwa kukemea kwake Bwana, Kwa mvumo wa pumzi ya puani mwake.
17 Alipeleka kutoka juu, akanishika; Akanitoa katika maji mengi;
18 Akaniokoa na adui yangu mwenye nguvu, Na wale walionichukia; Maana walikuwa na nguvu kuliko mimi.
19 Walinikabili siku ya msiba wangu; Lakini Bwana alikuwa tegemeo langu.
20 Akanitoa akanipeleka panapo nafasi; Aliniponya kwa kuwa alipendezwa nami.
21 Bwana alinitendea sawasawa na haki yangu; Sawasawa na usafi wa mikono yangu akanilipa.
22 Maana nimezishika njia za Bwana, Wala sikumwasi Mungu wangu.
23 Maana hukumu zake zote zilikuwa mbele yangu; Na kwa habari za amri zake, sikuziacha.
24 Nami nalikuwa mkamilifu kwake, Nikajilinda na uovu wangu.
25 Basi Bwana amenilipa sawasawa na haki yangu; Sawasawa na usafi wa mikono yangu mbele zake.
26 Kwa mtu mwenye fadhili utakuwa mwenye fadhili Kwa mkamilifu utajionyesha kuwa mkamilifu;
27 Kwake ajitakasaye utajionyesha kuwa mtakatifu; Na kwa mpotovu utajionyesha kuwa mkaidi.
28 Na watu wanaoonewa wewe utawaokoa; Ila macho yako ni juu ya wenye kiburi, uwadhili.
29 Kwa kuwa wewe u taa yangu, Ee Bwana; Na Bwana ataniangazia giza langu.
30 Maana kwa msaada wako nafuatia jeshi; Kwa msaada wa Mungu wangu naruka ukuta.
31 Mungu njia yake ni kamilifu; Ahadi ya Bwana imehakikishwa; Yeye ndiye ngao yao Wote wanaomkimbilia.
32 Maana ni nani aliye Mungu, ila Bwana? Ni nani aliye mwamba, ila Mungu wetu?
33 Mungu ndiye ngome yangu yenye nguvu; Naye huwaongoza wakamilifu katika njia yake.
34 Huifanya miguu yangu kuwa kama ya kulungu; Na kunisimamisha mahali pangu pa juu.
35 Ananifundisha mikono yangu vita; Hata mikono yangu yaupinda upinde wa shaba.
36 Nawe umenipa ngao ya wokovu wako; Na unyenyekevu wako umenikuza.
37 Umezifanyizia nafasi hatua zangu, Wala miguu yangu haikuteleza.
38 Nimewafuatia adui zangu, na kuwaangamiza; Wala sikurudi nyuma hata walipokomeshwa.
39 Nami nimewakomesha na kuwapiga-piga wasiweze kusimama; Naam, wameanguka chini ya miguu yangu.
40 Maana umenifunga mshipi wa nguvu kwa vita; Umenitiishia chini yangu walioniondokea.
41 Naam, adui zangu umewafanya wanipe visogo, Ili niwakatilie mbali wanaonichukia.
42 Walitazama, lakini hakuna wa kuokoa; Walimwita Bwana, lakini hakuwajibu.
43 Ndipo nikawaponda kama mavumbi ya nchi, Nikawakanyaga kama matope ya njiani, nikawatawanya.
44 Nawe umeniokoa na mashindano ya watu wangu; Umenihifadhi niwe kichwa cha mataifa; Watu nisiowajua watanitumikia.
45 Wageni watanijia wakinyenyekea; Kwa kusikia tu habari zangu, Mara watanitii.
46 Wageni nao watatepetea, Watatoka katika ngome zao wakitetemeka.
47 Bwana ndiye aliye hai; Na ahimidiwe mwamba wangu; Na atukuzwe Mungu wa mwamba wa wokovu wangu;
48 Naam, Mungu anipatiaye kisasi, Na kuwatweza watu chini yangu,
49 Na kunileta nje nitoke kwa adui zangu; Naam, waniinua juu yao walioniinukia; Waniponya na mtu wa jeuri.
50 Basi, Bwana, nitakushukuru kati ya mataifa, Nami nitaliimbia jina lako.
51 Ampa mfalme wake wokovu mkuu; Amfanyia fadhili masihi wake Daudi na mzao wake ,hata milele.