0:00
0:00

Mlango 14

Ninyi mmekuwa wana wa Bwana, Mungu wenu; msijitoje miili yenu, wala msifanye upaa katikati ya macho yenu kwa ajili ya aliyekufa.
2 Kwa kuwa u taifa takatifu kwa Bwana, Mungu wako, na Bwana amekuchagua kuwa watu wake hasa, kuliko mataifa yote yaliyo juu ya uso wa nchi.
3 Usile kitu cho chote kichukizacho.
4 Wanyama mtakaokula ni hawa ng'ombe, na kondoo, na mbuzi,
5 kulungu, na paa, na kongoni, na mbuzi wa mwitu, na paa mweupe, na pofu, na mbuzi wa mlima;
6 na kila mnyama aliyepasuliwa ukwato, ukapasuka ukwato wake zikawa mbili, naye ni mnyama mwenye kucheua akatafuna tena, katika wanyama wote, ndiye mnyama mtakayemla.
7 Lakini, hawa msile katika wale wenye kucheua, na hao waliopasuliwa ukwato; ngamia, na sungura, na kwang'a, kwa kuwa hucheua, lakini hawakupasuliwa kwato, ni najisi kwenu;
8 na nguruwe, kwa kuwa amepasuliwa ukwato lakini hacheui, huyu ni najisi kwenu msile nyama zao, wala mizoga yao msiiguse.
9 Mtakula hawa katika wote walio majini; kila kilicho na mapezi na magamba mtakula;
10 na kila kisichokuwa na mapezi na magamba msile; ni najisi kwenu.
11 Mna ruhusa kula katika nyuni wote walio safi.
12 Lakini hawa msiwale; tai, na furukombe, na kipungu;
13 na kengewa, na kozi, na mwewe kwa aina zake;
14 na kila kunguru kwa aina zake;
15 na mbuni, na kirukanjia, na dudumizi, na kipanga kwa aina zake;
16 na bundi, na mumbi, na bundi mkubwa;
17 na mwari, na nderi, na mnandi;
18 na membe, na koikoi, kwa aina zake; na hudihudi, na popo.
19 Na wadudu wote watambaao wenye mabawa ni najisi kwenu; msiwale.
20 Mna ruhusa kula katika nyuni wote walio safi.
21 Msile nyamafu yo yote; waweza kumpa mgeni aliye ndani ya malango yako, ili apate kula; au kumliza mtu wa mataifa; kwa kuwa wewe u taifa takatifu kwa Bwana, Mungu wako. Usimtokose mwana-mbuzi katika maziwa ya mamaye.
22 Usiache kutoa zaka ya fungu la kumi katika maongeo yote ya mbegu zako, yatokayo shamba mwaka baada ya mwaka.
23 Nawe utakula mbele za Bwana, Mungu wako, mahali atakapochagua apakalishe jina lake, zaka ya nafaka zako, na divai yako, na mafuta yako, na wazaliwa wa kwanza wa makundi yako ya ng'ombe na ya kondoo; ili upate kujifunza kumcha Bwana, Mungu wako, daima.
24 Na njia ikiwa ndefu mno nawe, usiweze kuzichukua kwa kuwa mahali ni mbali nawe mno atakapochagua Bwana, Mungu wako, apakalishe jina lake, hapo atakapokubarikia Bwana, Mungu wako;
25 ndipo uzibadili ziwe fedha, na kufunga zile fedha uende nazo mkononi mwako, hata mahali atakapochagua Bwana, Mungu wako;
26 na zile fedha zitumie kwa cho chote itakachotamani roho yako, ng'ombe, au kondoo, au divai, au kileo, au roho yako itakacho kwako cho chote; nawe utakula huko mbele za Bwana, Mungu wako; tena furahi, wewe na nyumba yako;
27 na Mlawi aliye ndani ya malango yako usimwache, kwani hana fungu wala urithi pamoja nawe.
28 Kila mwaka wa tatu, mwisho wake, toa fungu la kumi lote la maongeo yako ya mwaka huo, uliweke ndani ya malango yako;
29 na Mlawi kwa kuwa hana fungu wala urithi pamoja nawe, na mgeni, na yatima, na mjane aliyefiliwa na mumewe, walio ndani ya malango yako, na waje wale na kushiba; ili kwamba Bwana, Mungu wako, akubarikie katika kazi yote ya mkono wako uifanyayo.